Shahidi akwamisha kesi ya Maimu wa Nida

Muktasari:

  • Kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa mkurugenzi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida), Dickson Maimu na wenzake wanne katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imekwama kusikilizwa baada ya upande wa mashtaka kutokuwa na shahidi

Dar es Salaam. Kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa mkurugenzi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida), Dickson Maimu na wenzake wanne katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imekwama kusikilizwa baada ya upande wa mashtaka kutokuwa na shahidi.

Leo Jumatano Januari 15, 2020 wakili wa Serikali mkuu, Zacharia Ndaskoi ameeleza hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Salum Ally akibainisha kuwa kesi hiyo ilipangwa kwa ajili ya kuanza kusikiliza ushahidi wa upande wa mashtaka.

“Ila shahidi tuliyemtarajia kuanza kutoa ushahidi hatujampata, “amesema wakili Ndaskoi na kuiomba mahakama  kuahirisha kesi hiyo, kuipangia tarehe nyingine ianze kusikilizwa mfululizo.

Wakili wa utetezi, Joseph Ndunguru amesema hana pingamizi na ombi hilo, “lakini kwa kuwa tuliambiwa kesi  ina mashahidi 60 na vielelezo 200 tunaomba mashahidi waletwe wengi siku hiyo.”

Baada ya kutolewa kwa hoja hizo, Hakimu Ally ameahirisha kesi hiyo hadi Januari 27, 2020.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni meneja biashara wa Nida, Aveln Momburi; ofisa usafirishaji, George Ntalima; mkurugenzi wa sheria, Sabina Raymond na Xavery Kayombo.

Miongoni mwa mashtaka yanayowakabili ni kuisababishia Serikali hasara ya Sh1.175 bilioni, utakatishaji fedha, kughushi, kuwasilisha nyaraka za uongo ili kumdanganya mwajiri wao  na kuisababishia mamlaka hiyo hasara, kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu na matumizi mabaya ya madaraka.