Simbeye asema taasisi za Serikali zinalalamikia mazingira ya biashara

Muktasari:

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi nchini Tanzania (TPSF), Godfrey Smbeye amesema hivi sasa wanaolalamika urasimu kwenye mazingira ya biashara ni taasisi za Serikali na sio sekta binafsi.

Dar es Salaam. Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi nchini Tanzania (TPSF), Godfrey Simbeye amesema hivi sasa wanaolalamika urasimu kwenye mazingira ya biashara ni taasisi za Serikali na sio sekta binafsi.

Simbeye amesema hayo leo Jumapili Februari 16, 2020 kwenye kongamano maalumu la uwekezaji lililofanyika  mjini Vwawa mkoani Songwe lililoandaliwa mahsusi kwa ajili ya kutangaza fursa zilizoko kwenye mkoa huo.

Amesema hivi sasa wanalalamikia kwenye mazingira ya biashara ni taasisi za Serikali kuliko sekta binafsi

“Sasa hivi kinachotokea ndani ya Serikali tumefika mahali watu ambao wanalalamikia procedure ndefu za kufanya biashara Tanzania ni public sectors, yaani Serikali ndio wanaolalamika sasa wakati huko nyuma sisi ndio tuliokuwa tunalalamika sasa imegeuka” amesema bosi huyo wa TPSF.

“Wanalalamika kuwa hizi taratibu tulizokuwa tumeziweka huko nyuma hazitusaidii kwenda mbele”

Amesema kuwa jambo kubwa ambalo wao kama TPSF wanaloliona kipindi hiki ni mabadiliko ya fikra

“TPSF tuna jambo ambalo watu wengi hawalioni, kuna kitu kinatokea ndani ya nchi hii ambacho ni mabadiliko ya fikra.”

Amesema kuna maendeleo ya miundombinu kwa ajili ya kuvutia wawekezaji lakini fikra za wanaotaka kuwekeza bado ni za zamani.

 “Rais amefanya jambo zuri sana kwa sababu huwezi kujenga SGR (reli ya kisasa) kwa ajili ya kuvutia wawekezaji, Halafu fikra za kuwasaidia wale wanaotaka kuwekeza bado ni zile za zamani,” amesema.