Spika Ndugai kuwataja wabunge waliotelekeza watoto
Muktasari:
Spika wa Job Ndugai amesema anayo orodha ya wabunge waliotelekeza watoto, lakini Waziri Kangi Lugola amewataka wanawake kurudi nyumbani kumenoga
Dodoma. Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai amepanga kuwaanika hadharani wabunge waliotelekeza watoto akisema siku hiyo hapatatosha.
Ndugai ametoa kauli hiyo leo Jumatano Aprili 03, 2019 akiunga mkono majibu ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola ambaye amesema kuna watoto wanafanana na baadhi ya watu ndani ya Bunge.
"Hata mimi nina mawasiliano kadhaa na wanawake nchini wakiwalalamikia baadhi ya wabunge kuwa wametelekeza watoto, kuna siku nitakuja na orodha hapa mjue hapatatosha," amesema Ndugai
Akijibu swali la nyongeza la Tauhida Gallos (Viti Maalumu CCM), Waziri Lugola amewataka wanawake nchini kutoa malalamiko pale wanapohisi kutelekezewa watoto kwa kutumia Sheria ya Kanuni za Adhabu Sura 16 (166)
Hata hivyo, Waziri amewashauri wanawake kutumia kilichochao kwa maana ya kuzaa na Watanzania badala kuangalia wageni huku akisema 'rudini nyumbani kumenoga'.