VIDEO: Sumaye asababisha mmoja kujiuzulu uongozi Chadema

Waziri Mkuu mstaafu wa Tanzania, Frederick Sumaye akitangaza kukihama chama cha chadema alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Kushoto ni Katibu wa Chadema Kanda ya Pwani, Casmir Mabina ambaye naye amewasilisha barua ya kujiuzulu uongozi, kubaki kuwa mwanachama wa kawaida. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

Katibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Kanda ya Pwani, Casmir Mabina amewasilisha barua ya kujiuzulu uongozi, kubaki kuwa mwanachama wa kawaida.

Dar es Salaam. Katibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Kanda ya Pwani, Casmir Mabina amewasilisha barua ya kujiuzulu uongozi, kubaki kuwa mwanachama wa kawaida.

Mabina ameeleza uamuzi wake huo leo Jumatano Desemba 4, 2019 katika mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo uliitishwa na waziri mkuu mstaafu, Frederick Sumaye aliyetangaza  kuanzia leo kuwa si mwanachama wa Chadema, hatojiunga na chama kingine cha siasa, atabaki kuwa mshauri.

Sumaye ameponda hali ilivyokuwa katika uchaguzi wa uenyekiti Kanda ya Pwani ambao alipigiwa kura 48 za hapana kati ya kura 76, kwamba uliandaliwa mpango wa kumuangusha.

Baada ya Sumaye kumaliza kuzungumza, Mwananchi lilizungumza na Mabina kujua sababu za kuwepo katika mkutano wa Sumaye anayelalamika uchaguzi wa Kanda ya Pwani ambao yeye ndio alikuwa mmoja wa wasimamizi, “yametokea ndani ya eneo langu la kazi na kwa maana hiyo leo Jumatano nimewasilisha barua ya kujiuzulu nafasi yangu."

"Nitabaki kuwa mwanachama mwaminifu wa chama chetu na nitakuwa tayari kutoa ushirikiano wowote utakaohitajika.”