Tigo yazindua huduma itakaochochea mageuzi kwenye biashara

Mkurugenzi Mkuu wa MIC  Tanzania Simon Karikari akihutubia kwenye uzinduzi wa Tigo Business

Kampuni ya mawasiliano ya Tigo kupitia kitengo cha ‘Tigo Business’ jana imezindua huduma na bidhaa zilizoboreshwa zaidi pamoja na tovuti inayompa mteja mamlaka ya kujihudumia na kudhibiti matumizi ikiwa na lengo la kuzisaidia makampuni kukuza huduma zao kidigitali.

Aidha tovuti hiyo itawasaidia wateja kujua matumizi yao kwa wakati na kuwapa wateja mamlaka ya kusimamia akaunti zao.

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi, Mkurugenzi mkuu wa Tigo, Simon Karikari alisema Tigo business ni huduma inayokua kwa kasi ikiwalenga hasa wafanyabiashara na inaongoza katika huduma zenye ubunifu kwenye soko la mawasiliano.

Karikari alisema Tigo kama kampuni ya kidigitali ipo mstari wa mbele katika ukuzaji wa teknolojia na kuwa imejidhatiti katika kuhakikisha kampuni zinafikia malengo ya kutoa huduma zao kidigitali sokoni.

 “Bidhaa zetu ni pamoja na huduma za sauti, data, IoT pamoja na jumbe (Bulk SMS) zinazomruhusu mteja kuwasiliana na wateja wake kwa viwango nafuu.Tovuti hii pia inatoa intaneti mahsusi kwa kampuni ambazo zinahitaji suluhisho kubwa ili kuongeza ufanisi kwenye taasisi. Biashara ambazo zina matawi mengi zinaweza kuunganisha data, mifumo yake na uendeshaji kwa kutumia huduma ya ‘inter-branch connectivity solutions” aliongeza Karikari.

Tigo business inamiliki na kuendesha kituo cha data cha Kimataifa (Tier III Certified Data Center) Tanzania, kinachoruhusu kampuni za ndani kuhifadhi data zao na programu za biashara kwa usalama kupitia miundombinu iliyothibitishwa na mamlaka za kimataifa.

“Ukweli ni kwamba tunaishi kwenye dunia ambayo taarifa au data zina thamani hivyo zinahitaji kuhifadhiwa na kuchakatwa kwa ufanisi mkubwa ili kusaidia kampuni kufikia malengo ya biashara na ndiyo maana Tigo business imewekeza katika kuhakikisha inatoa suluhisho zenye kukidhi mahitaji na bajeti za kampuni,” alisema.

Pia kupitia miundombinu yenye usalama Tigo inatoa uhuru kwa wateja kuunganishwa na huduma za uhakika kupitia kwa watoa huduma wengine au moja kwa moja na Tigo na pia inatoa uhakika wa huduma kwa asilimia 99.9 hivyo kuzifanya biashara kuzalisha zaidi jambo linalochochea ukuaji.