Tshisekedi: Wengi walitarajia machafuko nilipochaguliwa

Muktasari:

Rais wa Congo, Felix Tshisekedi amesema baada ya kuchaguliwa kwake kuiongoza nchi hiyo watu wengi walidhani taifa hilo litaingia katika vurugu.


Dar es Salaam. Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Felix Tshisekedi amesema kuchaguliwa kwake kuwa rais ni tukio la kihistoria tangu nchi yake kupata uhuru mwaka 1960, ingawa watu wengi walitarajia vurugu kutokea.

Amesema yote yaliyotokea sifa zinapaswa kwenda kwa Rais mstaafu wa nchi hiyo, Joseph Kabila kwa sababu alifanya kazi kubwa ya kuimarisha demokrasia.

Ameyasema hayo leo Juni 13, 2019 Ikulu jijini Dar es Salaam wakati akizungumza katika hafla aliyoandaliwa na mwenyeji wake, Rais wa Tanzania, John Magufuli katika ziara yake ya siku mbili.

Amesema kwa mara ya kwanza, Januari 24 mwaka huu nchi hiyo iliingia katika historia ya kubadilishana madaraka kwa Amani, jambo ambalo halijawahi kutokea.

“Mabadilishano hayo yamefanyika kwa amani kabisa, watu wengine walikuwa hawaamini kwa sababu walikuwa wakisubiri yatokee machafuko baada ya uchaguzi mkuu lakini tangu tukio hilo tuna amani kama ilivyo Tanzania,” amesema Tshisekedi.

Amesema baada ya kubadilishana madaraka kwa amani suala lililobakia ni kuhakikisha nchi hiyo inakuwa na usalama hivyo amemwomba Rais Magufuli amshauri namna nzuri ya kufikia suala hilo.

“Nachukua fursa hii kuwashukuru wanajeshi wa Tanzania waneoendelea kulinda amani juu ya nchi ya Congo, kitendo hiki kinaonyesha ni jinsi gani Tanzania iko kwa karibu sana na nchi yetu,” amesema Tshisekedi.