Uhamiaji yaeleza sababu za kumzuia Zitto asitoke nje ya Tanzania

Kiongozi wa ACT- Wazalendo, Zitto Kabwe 

Muktasari:

Kiongozi wa ACT- Wazalendo, Zitto Kabwe jana Jumanne alizuia kusafiri kwenda nchini Kenya na Idara ya Uhamiaji Zanzibar kwa madai kwamba mwanasiasa huyo hatakiwa kutoka nje ya Tanzania


Unguja. Idara ya Uhamiaji Zanzibar imesema kuzuiliwa kusafiri nje ya nchi kwa Kiongozi wa ACT- Wazalendo Zitto Kabwe kunatokana na agizo la Serikali ya Tanzania.

Msemaji wa Uhamiaji Zanzibar, Sharif Bakar Sharif ametoa kauli hiyo leo Jumatano Juni 12, 2019 wakati akizungumza na Mwananchi Mjini Unguja, Zanzibar

Amesema kilichofanywa na Uhamiaji ni kutekeleza agizo Serikali la kumzuia baada ya kuonekana kuna haja ya kuzuiwa kwa mujibu wa taratibu ya vyombo vya ulinzi na usalama juu ya utekelezaji wa maagizo ya Serikali.

"Sisi kwa kuwa ni sehemu ya vyombo vya ulinzi na usalama tulitekeleza agizo hilo la kutomruhusu kusafiri nje ya Tanzania na tayari tumeshamfikisha katika vyombo vingine vya sheria kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria na kikanuni," amesema Sharif.

Zitto alikamatwa Jana Jumanne majira ya saa nane mchana, uwanja wa ndege Zanzibar wakati akiwa katika taratibu za kutaka kusafiri kwenda nchini Kenya.

Hata hivyo, jana jioni Zitto ambaye pia ni mbunge wa Kigoma Mjini aliachiwa na haijafahamika chanzo cha kuzuia kwake ni kipi.

Jana usiku, Mwananchi lilizungumza na Mwenyekiti kamati ya Itikadi, Mawasiliano na Uenezi wa chama hicho, Salim Bimani aliyedhibitishwa kukamatwa kwa Zitto na sababu za kuzuiwa kwake hawakuwa wanazifahamu.

Endelea kufuatilia Mwananchi kupata undani ya habari hii