Ulinzi ulivyokuwa mkutano wa Sumaye

Waziri Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Frederick Sumaye akiondoka katika chumba cha mkutano baada ya kutangaza kukihama chama cha Chadema katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

Ulinzi ulikuwa wa kutosha. Ndivyo unavyoweza kuuzungumzia ulinzi katika mkutano wa waziri mkuu mstaafu, Frederick Sumaye na waandishi wa habari uliofanyika leo Jumatano Desemba 4, 2019 katika jengo la LAPF Kijitonyama, jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Ulinzi ulikuwa wa kutosha. Ndivyo unavyoweza kuuzungumzia ulinzi katika mkutano wa waziri mkuu mstaafu, Frederick Sumaye na waandishi wa habari uliofanyika leo Jumatano Desemba 4, 2019 katika jengo la LAPF Kijitonyama, jijini Dar es Salaam.

Kulikuwa na askari watano ukumbini huku wengine wakiwa katika magari mawili nje ya jengo hilo la ghorofa zaidi ya 15.

Katika mkutano huo Sumaye ametangaza kuwa si mwanachama tena wa Chadema, moja ya sababu za kuachana  na  chama hicho kikuu cha upinzani nchini ni kutozingatiwa kwa taratibu za uchaguzi wa uenyekiti Kanda ya Pwani.

Katika uchaguzi wa Kanda ya Pwani, Sumaye alipigiwa kura 48 za hapana kati ya 76, kubainisha kuwa kuna watu waliandaliwa kumuangusha huku akimtaka mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kumaliza makundi ndani ya chama hicho.

Katika mkutano huo uliofanyika ghorofa ya 14, ukumbini kulikuwa na askari polisi watano  huku wengine wakiwa chini wakizunguka huku na kule.

Sumaye alipomaliza kuzungumza na waandishi wa habari, walimsindikiza mpaka kwenye lifti na kuondoka eneo hilo na kufuatiwa na magari mawili ya polisi ambayo hayakufuatana naye.