VIDEO: Kikwete ataja sifa za Nyerere

VIDEO: Kikwete ataja sifa za Nyerere

Muktasari:

Kongamano la miaka 20 ya kifo cha Mwalimu Nyerere limefanyika katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.


Dar es Salaam. Rais mstaafu wa Tanzania, Jakaya Kikwete amesema mwalimu Julius Nyerere amefariki akiacha Taifa lenye amani na mshikamano.

Ametoa kauli hiyo leo Jumanne Oktoba 8, 2019  katika kongamano la kumbukumbu ya miaka 20 ya kifo cha baba huyo wa Taifa la Tanzania lililofanyika katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Kigamboni, Dar es Salaam.

Rais huyo wa Awamu ya Nne amesema Nyerere alionyesha moyo wa kujitolea, alipoacha kazi ya kuajiriwa na kwenda kupigania uhuru kupitia chama cha TANU.

"Alijaliwa karama ya kupigania uhuru kwa maneno bila kutumia nguvu za kijeshi na kumwaga damu," amesema Kikwete.

Ametaja sifa yake nyingine ni kitendo cha kuunganisha Tanganyika na Zanzibar akishirikiana na Rais mstaafu wa  Zanzibar, Abeid Aman Karume.

Amesema aliona uhuru wa Tanganyika haukuwa na maana kama nchi nyingine za Afrika hazitakuwa huru.

"Alipenda vijana na ndio maana alianzisha nafasi za vijana katika halmashauri kuu ya TANU na baadaye CCM. Mimi mwenyewe nilipata nafasi. Alianza na nafasi tano baadaye zikafika 10. Aliamini kuwa suluhu inapatikana kwa mazungumzo,” amesema.