Vyama 2,000 vya akiba na mikopo hatarini kufutwa

Muktasari:

Vyama vya ushirika vya akiba na mkopo zaidi ya 2,000 nchini Tanzania hatarini kufutwa kutokana na kutokuwa na anuani jambo ambalo linatia shaka kuanzishwa kwake.

Arusha. Vyama vya ushirika vya akiba na mkopo zaidi ya 2,000 nchini Tanzania hatarini kufutwa kutokana na kutokuwa na anuani jambo ambalo linatia shaka kuanzishwa kwake.

Hayo yameelezwa leo Jumatano  Oktoba 9, 2019 na mrajisi wa vyama vya ushirika nchini Tanzania, Tito  Haule wakati akizungumza katika maadhimisho ya  siku ya kimataifa ya ushirika wa  akiba na mkopo.

Amesema vyama vya ushirika kwa sasa vipo 6,137  lakini zaidi ya 2,000 havifanyi kazi ipasavyo.

Haule amezitaka bodi kuhakikisha sheria za ushirika zinafuatwa,  mikutano inafanyika kwa mujibu wa sheria kuhakikisha fedha za vyama vya ushirika zinalindwa.

"Kuna chama cha ushirika kilifanya  vikao 25 kwa mwaka na kila kikao mshiriki analipwa  Sh300,000 wakati sheria inasema vikao vifanyike  mara nne kwa mwaka.”

“Na ikitokea  dharura  viongezwe viwili tu ili jumla viwe sita, lazima vyama vya ushirika  vijue wakati wa mkutano," amesema  Haule

Makamu Mwenyekiti wa vyama  vya ushirika nchini Tanzania, Somoi Ismail amesema licha ya kuwa kuna changamoto katika vyama  bado kuna mwamko kuhusu vyama vya ushirika kutokana na vingi kushiriki maadhimisho hayo.

Willbard Gereki, mshiriki wa  amesema kuwa mafunzo yamewapa uelewa na hakuna mwananchi atakaye omba mkopo akakosa kutokana na usimamizi mzuri wa serikali.