Waitara atangaza kumvaa John Heche Tarime vijijini

Muktasari:

  • Mwaka 2020 Tanzania inafanya uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais ambapo baadhi ya watia nia wameanza kujitokeza kutia nia na miongoni ni mbunge wa sasa wa Ukonga (CCM), Dar es Salaam, Mwita Waitara ambaye amesema iwapo chama chake kitampitisha atagombea ubunge Tarime Vijijini mkoani Mara.

Dar es Salaam. Mbunge wa Ukonga (CCM), jijini Dar es Salaam nchini Tanzania, Mwita Waitara ametangaza katika uchaguzi mkuu 2020, atagombea ubunge Tarime Vijijini mkoani Mara.

Uamuzi huo wa Waitara ameutangaza hivi karibuni akiwa Tarime ikiwa ni ishara kwamba hatogombea tena Ukonga kama alivyofanya mwaka 2015 akiwa Chadema kabla ya kujiuzulu na kutimkia CCM mwaka 2018 alikopitisha kutetea nafasi hiyo na akashinda.

Jimbo la Tarime Vijijini kwa sasa linaongozwa na John Heche wa Chadema.

Waitara ambaye pia ni Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais- Tamisemi amesema ametia nia ya kugombea ubunge katika jimbo hilo na atafurahia endapo Chadema itampitisha tena Heche kugombea ili aweze kuchuana naye.

Naibu waziri huyo ametangaza nia hiyo wakati akisherehekea sikukuu ya mwaka mpya na wakazi wa Tarime vijijini sehemu ambayo wazazi wake wanaishi.

Akizungumza katika hafla, Waitara alisema ikitokea ikawapendeza wajumbe wa mkutano mkuu wa chama jimbo, kamati ya siasa ya wilaya, kamati ya siasa ya mkoa, wajumbe wa halmashauri kuu ya CCM na kamati kuu wakampitisha atakuwa mgombea ubunge.

“Naiomba Chadema imlete John Heche hapa Tarime Vijijini tukutane, nimesikia anataka kwenda mjini asiende,” alisema Waitara

Alisema kwa mara ya kwanza aligombea  jimbo hilo mwaka 2010 akiwa CCM lakini kutokana yeye kuwa masikini alikosa fursa hiyo.

“Wakati huo utaratibu wao ulikuwa mwenye pesa ndiye hupewa nafasi, sikuwa na pesa wala mdhamini ina maana katika familia hii niliingia katika siasa peka yangu, sina shangazi, sina mjomba mimi ni jeshi la mtu mmoja, katika mazingira hayo yaliyotokea yalinifanya mimi kuhama chama wakati ule,” alisema Waitara 

Alisema mwaka 2010 alirudi katika jimbo hilo na kuomba ubunge, kazi ikafanyika lakini haikuwezekana, labda Mungu hakupenda jambo ambalo lilimfanya kwenda kuwa mwenyekiti wa mtaa wa Kivule katika jimbo la Ukonga jijini Dar es Salaam.

“Mwaka 2015 nikagombea ubunge kupitia Chadema katika jimbo la Ukonga nikashinda lakini sasa nataka kurudi nyumbani,” alisema Waitara

Jitihada za kumpata Heche zinaendelea.