Wanafunzi kumi bora wavulana matokeo darasa la saba watoka kanda ya ziwa

Muktasari:

  • Mikoa ya kanda ya ziwa yaongoza katika ufaulu wa wavulana matokeo ya mtihani wa darasa la saba uliofanyika mwaka 2019 ambapo wanafunzi kumi bora kwa wavulana wametoka mikoa ya kanda ya ziwa.

Dar es Salaam. Baraza la Mitihani la Taifa la Tanzania (NECTA) limetangaza matokeo ya mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi ambako mikoa ya kanda ya ziwa imeonekana kuongoza kwa kushika nafasi zote 10 bora kwa wavulana.

Katika matokeo hayo yaliotangazwa leo Jumanne Oktoba 15, 2019 nafasi ya kwanza hadi ya 10 katika orodha ya wavulana waliofanya vizuri zimeshikwa na wanafunzi kutoka katika mikoa ya kanda ya ziwa.

Nafasi ya kwanza imekwenda kwa Francis Gwaji kutoka shule ya Paradise ya mkoa wa Geita, wakati nafasi ya pili hadi ya nne ilichukuliwa na wanafunzi wa shule ya Graiyaki ya Mara ambao ni Victor Godfrey, Aziz Yassin na Goldie Hihayuma.

Nafasi ya tano imeshikwa na Daniel Daniel wa shule ya Little ya Shinyanga huku nafasi ya sita ikichukuliwa na Hilary Nassor wa shule Peaceland ya Mwanza.

Bado mikoa ya kanda ya ziwa imeendelea kutesa katika nafasi ya saba ambayo imeshikiliwa na Mbelele Mbelele wa Kwema Modern iliyopo Shinyanga, nafasi ya nane ikishikwa na Derick Lema wa shule ya Musabe mkoani Mwanza.

Namba tisa imechukuliwa na Athanas Sekuro wa Paradise ya Geita na dimba la wavulana kumi bora likifungwa na Aron Mabuga kutoka shule ya Kwema Modern ya Shinyanga.