Wananchi watakiwa kuzikimbilia ‘mahakama zinazotembea’ kueleza vilio vyao

Rais John Magufuli, Jaji Mkuu Ibrahim Juma, Waziri wa Sheria na Katiba, Profesa Palamagamba Kabudi, Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya dunia nchini, Bella Bird na Mkuu wa wilaya ya Ilala Sophia Mjema wakikata utepe kuzindua Mahakama inayotembea wakati wa maadhimisho ya wiki ya sheria nchini yanayofanyika jijini Dar es Salaam leo. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Ukonga, Faudhia Hamza amewataka wananchi wenye malalamiko na vinyongo kuvieleza katika mahakama zinazotembea.

Dar es Salaam. Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Ukonga, Faudhia Hamza amewataka wananchi wenye malalamiko na vinyongo kuvieleza katika mahakama zinazotembea.

Ametoa wito huo leo Alhamisi Septemba 12, 2019 katika mahakama hiyo Chanika, jijini Dar es Salaam.

Mahakama inayotembea huwa katika gari maalum lenye vifaa mbalimbali  kama televisheni, kamera zenye uwezo wa kurekodi ushahidi wote wa picha na sauti.

"Wananchi nawaomba mnapoiona hii gari ya mahakama inayotembea msiikimbie wala kufikiri kuwa sasa mtafungwa, huu ni ukombozi  wenu jitokezeni ili kutatua matatizo hasa yanayohusiana na madai, mirathi na ndoa,” amesema Hakimu Hamza.

Hakimu mkazi mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Martha Mpaze amesema mahakama hiyo inasikiliza kesi za madai, talaka na mirathi kwa kutoa usuluhishi zaidi.

Mkazi  wa Chanika, Yahaya Rajabu aliishukuru mahakama kwa kusogeza huduma mtaani kwa maelezo kuwa jambo hilo litasaidia wananchi kupata uelewa wa sheria kwa kuwa wengi wanakabiliwa na changamoto nyingi.