Wanandoa kutengewa eneo la kupiga picha daraja la Kigongo- Busisi

Muktasari:

  • Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole amesema katika daraja la Kigongo-Busisi linalojengwa mkoani Mwanza  litatengwa eneo maalum kwa ajili ya wanandoa kupiga picha.

Mwanza. Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole amesema katika daraja la Kigongo-Busisi linalojengwa mkoani Mwanza  litatengwa eneo maalum kwa ajili ya wanandoa kupiga picha.

“Tutatenga sehemu kwa ajili ya vijana wetu wanaofunga ndoa kupiga picha katika daraja la Kigongo- Busisi,” amesema Polepole katika sherehe za miaka 43 tangu kuanzishwa kwa CCM zilizofanyika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Amesema Watanzania wataanza kufanya sherehe ya ndoa ya aina yake kwa madai kuwa ujenzi wa daraja hilo utatoa nafasi kwa wanandoa kupiga picha nzuri kutokana na mwonekano wa eneo hilo.

Polepole amesema ilani ya uchaguzi ya CCM  inamtaka kiongozi kuhakikisha anatekeleza miradi yenye manufaa kwa wananchi, kwamba hicho ndicho kilichofanywa na mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli.

Amebainisha kuwa mambo yaliyofanywa na CCM yanaonekana kwa macho kwani miradi mingi inayotekelezwa na Serikali imeanza kuwanufaisha Watanzania.