Wapinzani Tanzania wahoji bajeti uendeshaji wa mapori yaliyopandishwa hadhi

Msemeji wa kambi ya upinzani, Catherine Ruge akisoma maoni ya kambi hiyo kuhusu azimio la kuridhia mapendekezo ya ubadilishaji wa sehemu za mapori ya akiba ya Kigosi na Ugalla kuwa hifadhi za Kigosi na Mto Ugalla, bungeni jijini Dodoma leo. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni nchini Tanzania imemtaka Waziri wa Maliasili na Utalii nchini,   Dk Hamis Kigwangala kulieleza Bunge ni fungu gani limeridhiwa na chombo hicho cha kutunga sheria kwa ajili ya uendeshaji wa Hifadhi za Kigosi na Ugalla.


Dodoma. Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni nchini Tanzania imemtaka Waziri wa Maliasili na Utalii nchini,   Dk Hamis Kigwangala kulieleza Bunge ni fungu gani limeridhiwa na chombo hicho cha kutunga sheria kwa ajili ya uendeshaji wa Hifadhi za Kigosi na Ugalla.

Hayo yameelezwa leo Jumanne Septemba 10, 2019 na  mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Catherine Ruge kwa niaba ya msemaji wa kambi hiyo wa Wizara ya Maliasili na Utalii.

Ruge alikuwa akisoma maoni ya kambi hiyo kuhusu Azimio la kuridhia mapendekezo ya ubadilishaji hadhi sehemu ya pori la akiba la Ugalla kuwa hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla na eneo la pori la Kigosi kuwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi.

Akisoma maoni hayo, Catherine amesema uamuzi huo unatolewa bila kuwepo kwa kasma ya uendeshaji, kwamba si kama unalisaidia Taifa kwani analazimika kunyang’anya fedha ambazo tayari zimeshapangiwa matumizi kwenye bajeti na kusababisha miradi mingine kusimama hadi uamuzi wa dharura utekelezwe.

“Ikumbukwe kuwa muda ni raslimali pindi unapopita haurudi tena na hiyo ni hasara ambayo haiwezi kufidiwa,” amesema.