Wapinzani waongoza kwa asilimia ya wanawake Bunge la Tanzania

Muktasari:

Spika wa bunge wa bunge Job Ndugai amesema asilimia za wabunge wanawake waliopitia bunge la Tanzania bado ni ndogo

Dodoma. Tangu Tanzania ipate Uhuru, wabunge wanawake kutoka upinzani wamefikia asilimia 40.3 huku wabunge wanawake wa CCM wakiwa  wamefikia asilimia 19.8.

Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai ameliambia bunge leo Jumanne Novemba 5, 2019 katika siku ya kwanza ya Bunge kuwa tangu uhuru  hadi sasa, Bunge la Tanzania limekuwa na jumla ya wabunge 3,041 na kati yao, wabunge wanawake ni 484 sawa na asilimia 15.

Spika Ndugai amesema tangu Uhuru hadi sasa, Chama cha Mapinduzi kina wabunge 1,294 na kati yao, wanawake ni 256 wakati upinzani wamefikia jumla ya wabunge 328 na kati yao wanawake ni 124.

“Bado safari ni ndefu sana, ukihesabu tangu Uhuru ambapo tulikuwa na wabunge wanawake 6 kati ya wabunge 81, lakini tunazidi kusonga mbele ingawa hatujafika kunakotakiwa,” amesema Ndugai.

Kwa mujibu wa kiongozi huyo, bado kuna haja ya kuongeza juhudi za idadi ya wabunge wanawake ndani ya bunge ili kuongeza asilimia.