VIDEO: Wasimamizi uchaguzi Serikali za Mitaa Dar waonywa

Mkuu wa Idara ya Elimu Msingi, Elizabeth Thomas, akiapa mbele ya Mwanasheria, Frank Mushi, kwa ajili ya kusimamia uchaguzi serikali za Mitaa.

Muktasari:

Walioteuliwa kusimamia uchaguzi wa Serikali za Mitaa jijini Dar es Salaam wametakiwa  kuhakikisha wanasimamia uchaguzi huo kwa kufuata sheria na sio utashi wao.

Dar es Salaam. Walioteuliwa kusimamia uchaguzi wa Serikali za Mitaa jijini Dar es Salaam wametakiwa  kuhakikisha wanasimamia uchaguzi huo kwa kufuata sheria na sio utashi wao.

Wito huo umetolewa leo Alhamisi Oktoba 12, 2019 na katibu tawala wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abubakar Kunenge  wakati wa kuapishwa kwa wasimamizi hao watakaosimamia uchaguzi  katika wilaya tano za mkoa huo.

Walioapishwa na wilaya kwenye mabano ni Kiduma Mageni,(Kinondoni), Salum Pawn(Temeke), Kissah Mbilla(Ubungo),Elizabeth Thomas(Ilala) na Charles Lawisso(Kigamboni).

Kunenge amewataka wasimamizi hao kutambua kuwa uchaguzi huo una sheria, kanuni na taratibu zake na wasingependa kuona mtu anaenda kinyume.

"Katika kueuliwa kwenu uchunguzi ulifanyika wa kina na kujua maadili mliyonayo, hatutarajii muende kinyume na yale yanayotakiwa katika uchaguzi huo, katendeni haki," amesema Kunenge.

Hakimu Mfawidhi Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni, Frank Mushi aliyewaapisha wasimamizi hao, amesema wamekula  viapo viwili katika utekelezaji wa kazi hiyo ikiwemo cha  uaminifu na kile cha utii na uadilifu.