VIDEO: Wazee wabariki Chadema kujitoa uchaguzi Serikali za mitaa

Muktasari:

Baraza la wazee la  Chadema limebariki uamuzi wa chama hicho kujitoa kushiriki uchaguzi wa Serikali za mitaa utakaofanyika Novemba 24, 2019.

Dar es Salaam. Baraza la wazee la  Chadema limebariki uamuzi wa chama hicho kujitoa kushiriki uchaguzi wa Serikali za mitaa utakaofanyika Novemba 24, 2019.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Ijumaa Novemba 8, 2019 mwenyekiti wa baraza hilo, Hashim Juma Issa amesema ilikuwa lazima chama hicho kijitoe kutokana na kutengenezewa mazingira ya kufanya hivyo.

“Naomba hilo suala lieleweke Chadema tumetolewa kwa hila za waziwazi na sisi tumeona tujitoe ili wafurahi wao hatuwezi kushiriki kwenye hujuma namna hii,” amesema.

Issa amekwenda mbali zaidi na kuwataka wanachama wao kote nchini kutotoa ushirikiano kwa viongozi watakaoteuliwa kushika nafasi mbalimbali kwenye uchaguzi huo.

“Hatuna sababu ya kushirikiana nao kwa kuwa wameteuliwa na sisi tunahitaji viongozi wa kuchaguliwa na wananchi kidemokrasia,” amesema.

Mwenyekiti huyo amesema Chadema waliweka misingi ya kufanya vyema katika uchaguzi huo.

Amebainisha kwamba kati ya watu 19 milioni waliojiandikisha wana uhakika asilimia 90 ni wafuasi wa chama hicho kikuu cha upinzani nchini.