Waziri Jafo: Uchaguzi serikali za mitaa Novemba 24

Muktasari:

Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Rais Tawala za Mkoa na Serikali za Mitaa( Tamisemi) Selemani  Jafo ametoa maelekezo na Tangazo la uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka 2019 kwa wakuu wa mikoa na wadau mbalimbali wa uchaguzi huo.

Dodoma. Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Selemani Jafo amesema uchaguzi wa serikali za mitaa utafanyika Novemba 24, 2019.

Jafo ametangaza tarehe ya uchaguzi huo leo Ijumaa Agosti 23, 2019 wakati wa mkutano wake na wakuu wa mikoa, makatibu tawala na wadau mbalimbali uliolenga kutoa maelekezo na tangazo la uchaguzi huo.

Amesema kwa mujibu wa kanuni za uchaguzi uandikishaji wapiga kura utaanza siku 47 kabla siku ya uchaguzi na utadumu kwa siku saba.

Amesema upigaji kura utaanza saa 2.00 asubuhi na kuhitimishwa saa 12.00 jioni.

Waziri Jafo amesema viongozi watakoma uongozi wao  siku saba kabla ya siku ya  kuchukua fomu za kugombea.

Amesema waangalizi wa uchaguzi wataruhusiwa baada ya kupata kibali kutoka kwa katibu mkuu Tamisemi na maombi yatatakiwa  kupata kibali kwa katiba mkuu ndani ya siku 21 baada ya tangazo la uchaguzi kutoka.

Amesema kampeni sitafanyika siku saba kabla ya tarehe ya uchaguzi wa serikali za mitaa.

Awali, Katibu Mkuu Tamisemi, Joseph Nyamuhanga amesema maandalizi muhimu katika uchaguzi huo yamekamilika.