Waziri Jafo awaita Dodoma Ma RC, RAS kuhusu uchaguzi serikali za mitaa

Muktasari:

Kesho Ijumaa, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Seleman Jafo atatoa tangazo la uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka 2019 jijini Dodoma ambapo amewaalika wakuu wa mikoa, katibu tawala na wadau mbalimbali kuhudhuria mkutano huo.


Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Seleman Jafo amewaita Wakuu wa Mikoa (RAS) na Makatibu Tawala wa mikoa (RAS) kwenda jijini Dodoma.

Pamoja na Ma RC, RAS kutoka mikoa 26 ya Tanzania Bara, Waziri Jafo amewaalika wadau wengine kuhudhuria mkutano wa kazi na viongozi hao wenye lengo la kutoa tangazo la uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka 2019.

Taarifa kwa umma iliyotolewa leo Alhamisi Agosti 22,2019 na Katibu Mkuu wa Tamisemi, Joseph Nnyamhanga amesema Waziri Jafo atatumia huo kutoa maelekezo mbalimbali kuhusu uchaguzi huo unaotarajia kufanyika Novemba 2019.

Jumatatu ya Agosti 19,2019, Waziri Jafo alisema wiki hii siku yoyote atatangaza tarehe maalum ya kufanyika kwa uchaguzi huo wa serikali za mitaa ambao hufanyika mwaka mmoja kabla ya uchaguzi mkuu.

Alisema kampeni za uchaguzi huo zikifanyika kwa siku saba kabla ya siku ya uchaguzi huku uandikishwaji wa wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi huo utafanyika siku 47 kabla ya uchaguzi.