Zimbabwe yatimua madaktari 200 waliogoma

Harare. Bodi ya Huduma za Afya nchini Zimbabwe (HSB) imetangaza kuwafukuza madaktari 211 kwa kushiriki mgomo wa kutaka maslahi zaidi.

Madaktari wamekutwa na hatia ya kutoonekana kazini bila kuwa likizo au sababu yoyote ya msingi kwa siku tano au zaidi, imesema taarifa ya HSB.

Mgomo huo ulianza Septemba mwaka huu.

HSB imesema madaktari 516 kati ya 1, 601 walioajiriwa na hospitali zinazofadhiliwa na serikali ama wamepata adhabu kutokana na mgomo huo.

Chama cha Madaktari cha Zimbabwe hakijazungumzia suala hilo, ingawa awali kililalamikia kuwapo vitisho, kwa mujibu wa BBC.

Mgomo umesababisha shughuli nyingi kukwama katika hospitali kwamba huduma za dharura pekee ndizo zinazotolewa.

Serikali haiwezi kumudu nyongeza ya mishahara wakati wananchi wanaitaka iharakishe kumaliza umasikini.

Zimbabwe iko katika hali ngumu kiuchumi na kushuka kwa thamani ya fedha zake, hali ambayo imeporomosha kipato cha wananchi.

Kiwango wanacholipwa madaktari wa nchi hiyo kwa dola za Zimbabwe ni sawa na Dola 100 za marekani  (Sh230,000) kwa mwezi, kiwango ambacho wanasema hakitoshi tena kwa chakula au pango.