Makonda aagiza kupulizwa dawa kuua vimelea vya virusi vya corona Dar

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda leo Machi 24, 2020 ameagiza kupulizwa dawa katika maeneo mbalimbali ya mkoa huo, ili kuua vimelea vya magonjwa ikiwemo virusi vya ugonjwa wa corona.
Makonda aliyasema hayo leo Jumanne Machi 24, 2020 alipotembelea stendi kuu ya Ubungo na kukagua kama watoa huduma hiyo ya usafiri nchini wameweka vitakasa mikono ili kujikinga na virusi vya corona.
Akiwa ameambatana na vyombo vya habari pia alitumia nafasi hiyo kuzungumza na abiria waliofika stendi hiyo kwa ajili ya kusafiri na kuwaelezea kuhusu hatari iliyopo ya ugonjwa huo duniani.
Makonda aliwataka abiria hao kuchukua tahadhari ili kujikinga kuambukiza wengine.
Amesema mkoa huo umeamua kuanzia wiki hii wataanza, kupuliza dawa kwenye maeneo mbalimbali ya jiji hilo ili kuua vimelea vya magonjwa mbalimbali ikiwemo virusi vya corona.
Makonda aliwataka wananchi kutoa taarifa mapema endapo wataona mtu mwenye dalili zinazofanana na zile za ugonjwa wa corona ili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa.