Keffe D kufikishwa mahakamani Agosti 10, mauaji ya Tupac
Muktasari:
- Tupac alifariki dunia Septemba 13, 1996, siku sita baada ya kupigwa risasi mjini Las Vegas, tukio lililotikisa tasnia ya muziki wa Hip Hop na kuacha maswali mengi yasiyo na majibu kwa miongo kadhaa.
Marekani. Ikiwa ni zaidi ya miaka 27 tangu kuuawa kwa rapa wa Marekani, Tupac Shakur. Hatimaye mwanga unaanza kuonekana katika kesi yake ambayo kwa muda mrefu imekuwa gumzo duniani.
Mahakama ya Jimbo la Nevada imepanga kuanza kusikiliza kesi hiyo Agosti 10, 2026, ikimhusu Duane “Keffe D” Davis, mtu pekee aliyekamatwa na kushtakiwa kwa madai ya kuhusika na mauaji ya msanii huyo.
Tupac alifariki dunia Septemba 13, 1996, siku sita baada ya kupigwa risasi mjini Las Vegas, tukio lililotikisa tasnia ya muziki wa Hip Hop na kuacha maswali mengi yasiyo na majibu kwa miongo kadhaa.
Duane “Keefe D” Davis, kiongozi wa zamani wa genge la ‘South Side Compton Crips (SSCC)’ ambaye ni mshukiwa wa kwanza katika kesi ya Tupac aliwahi kukiri hadharani kuhusika kwake katika tukio la ufyatuaji wa risasi mwaka 1996 kupitia kitabu chake (Memoir) na mahojiano mbalimbali.
Waendesha mashtaka wanadai Davis alikuwa “shot caller” yaani mtu aliyepanga na kuamuru shambulio la risasi lililotokea Las Vegas. Inadaiwa tukio hilo lilichochewa na ugomvi uliotokea ndani ya kasino, uliomhusisha Tupac Shakur na Orlando Anderson, ambaye ni mpwa wa Davis.
Aidha upande wa utetezi wa Davis mwaka 2025 uliwasilisha maombi la kuzuia ushahidi wakidai kuwa kesi haiwezi kutegemea matamko ya zamani ya Keefe D ambayo yalitolewa chini ya makubaliano ya kinga ya taarifa (immunity), na kwamba hakuna ushahidi wa moja kwa moja unaomuweka mahali pa tukio kama gari au bunduki yake.
Awali kesi hiyo ilipangwa kusikilizwa Februari 9, 2026, lakini imesogezwa mbele hadi Agosti 10, 2026 baada ya Jaji wa Mahakama ya Wilaya, Carli Kierny, kuridhia ombi hilo. Huku upande wa mashtaka na utetezi wakikubaliana kupata muda kidogo wa kuchambua nyaraka na ushahidi uliopo dhidi ya mteja wao.
Agosti 10 na Tupac
Baadhi ya mashabiki katika mitandao ya kijamii wamekuwa wakiihusisha tarehe hiyo kubwa ya kusikilizwa kwa kesi pamoja na mambo ambayo Tupac amewahi kuyafanya katika terehe hiyo enzi za uhai.
Agosti 10, 2004 Albamu ya moja kwa moja (live album) ya 2Pac Live, iliyokuwa na rekodi kutoka enzi ya albamu ya All Eyez on Me, ilipangwa kutolewa siku hiyo, lakini ilisogezwa mbele baada ya nyimbo zake kuvuja mitandaoni.
Agosti 10, 1984 Tupac, ambaye wakati huo alijulikana kama Lesane Parish Crooks, alifanya onyesho lake la kwanza jukwaani akicheza nafasi ya Travis katika tamthilia A Raisin in the Sun huko Baltimore, kulingana na simulizi za mashabiki.