Rais Tinubu wa Nigeria aahidi kuimarisha usalama

Bola Tinubu akiapishwa kuwa Rais wa Nigeria kufuatia ushindi alioupata katika sherehe zilizofanyika kwenye Uwanja wa Eagle Square Jijini Abuja leo Jumatatu Mei 29, 2023.

Muktasari:

  • Bola Tinubu alitangazwa kuwa mshindi katika Uchaguzi Mkuu wa Februari 25, 2023 kwa kupata kura milioni 8.8 na kutimiza idadi ya kura inayohitajika kisheria ya theluthi mbili katika majimbo yote ya Nigeria.

Abuja. Rais mpya wa Nigeria, Bola Tinubu aliyeapishwa leo Mei 29, 2023 ameahidi kuunganisha Taifa hilo lenye watu wengi zaidi barani Afrika na kukabiliana na ukosefu wa usalama kama kipaumbele kikuu.

 Mzee huyo mwenye umri wa miaka 71, anamrithi jenerali wa zamani wa jeshi, Muhammadu Buhari (80) wa chama kimoja, ambaye anaondoka madarakani baada ya mihula miwili ya uongozi na kuiacha nchi inakabiliwa na matatizo ya kiuchumi na changamoto za kiusalama.

“Kama Rais wa Jamhuri ya Shirikisho la Nigeria nitatekeleza majukumu yangu na kufanya kazi zangu kwa uaminifu kwa uwezo wangu wote, kwa uaminifu na kwa mujibu wa katiba,” Tinubu alisema baada ya kuapishwa katika Uwanja wa Eagle Square uliopo jijini Abuja.

Viongozi wa kigeni na wawakilishi waliohudhuria sherehe hizo ni pamoja na marais Cyril Ramaphosa (Afrika Kusini), Paul Kagame (Rwanda), Samia Suluhu Hassan (Tanzania) na Nana Akufo-Addo (Ghana) pamoja na wawakilishi wa Marekani, Uingereza na China.

Kashim Shettima aliapishwa kama Makamu wa Rais, akichukua nafasi ya Yemi Osinbajo.

Wawili hao wa chama tawala cha APC walitangazwa washindi katika uchaguzi wa Februari 25, 2023 na kupata idadi kubwa zaidi ya kura ambazo zinafikia theluthi mbili katika majimbo ya Nigeria.

Hata hivyo, Tinubu alipata zaidi ya theluthi moja tu ya kura zote, jambo ambalo wachambuzi wa masuala ya siasa wanasema linamfanya awe na mamlaka dhaifu.

Viongozi wa upinzani wanapinga matokeo mahakamani wakidai yalikuwa na udanganyifu.

Katika hotuba yake ya kwanza, Tinubu anayejulikana nchini Nigeria kama “godfather" wa siasa nchini humo, alisisitiza kuwa atafanya kazi ya kuunganisha nchi.

“Iwe kutoka kwenye vijito vya Niger Delta, misitu mikubwa ya savana ya kaskazini, mji mkuu wenye shughuli nyingi wa Abuja au masoko yenye shughuli nyingi ya Onitsha, ninyi nyote ni watu wangu,” alisema Tinubu.

“Kama Rais wenu, nitakutumikia bila ubaguzi kwa yeyote, ila huruma na upendo kwa wote.”

Buhari, ambaye Tinubu amejigamba kuwa alisaidia kumweka madarakani mwaka 2015, aliahidi kukabiliana na ufisadi na ukosefu wa usalama akiwa madarakani lakini amewakatisha tamaa wengi.

Anamwachia mrithi wake deni linaloongezeka na mfumuko wa bei, pamoja na wasiwasi mkubwa juu ya mashambulizi yasiyokoma na utekaji nyara unaofanywa na makundi watu wenye silaha.

Rais aliyemaliza muda wake ameondoka Abuja kwenda kutumia muda katika shamba lake huko Daura, katika Jimbo la Katsina, karibu na mpaka na Niger.

Akihutubia umati uliovalia mavazi ya kitamaduni, Tinubu aliahidi kushughulikia ghasia zilizoenea ambazo hutokea karibu kila siku nchini kote.

“Usalama ndio utakaopewa kipaumbele cha kwanza cha utawala wetu kwa sababu hakuna ustawi au haki unaoweza kuwepo huku kukiwa na ukosefu wa usalama na vurugu,” alisema.

Vikosi vya jeshi kwa sasa vinapambana na magenge ya wahalifu wenye silaha kali na watekaji nyara katika majimbo ya kati na kaskazini-magharibi, wezi wa mafuta, maharamia na wanaotaka kujitenga katika eneo la kusini mashariki, na uasi wa kijihadi uliodumu kwa miaka 14 kaskazini mashariki.