TCRA yafafanua idadi ya laini za simu

TCRA yafafanua idadi ya laini za simu

Muktasari:

  • Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (TCRA) imefafanua matumizi ya idadi ya simu kwa mtandao husika wa simu, ikisema hakuna mpango wa Serikali kutunga sheria nyingine.

Dar es Salaam. Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (TCRA) imefafanua matumizi ya idadi ya simu kwa mtandao husika wa simu, ikisema hakuna mpango wa Serikali kutunga sheria nyingine.

Badala yake, TCRA katika taarifa iliyotolewa juzi Juni 9, 2021 kwa vyombo vya habari imesema; “Serikali inakusudia kutunga sheria ya kulinda taarifa binafsi kwa lengo la kuhakikisha taarifa binafsi na faragha za watu zinalindwa.”

TCRA imesema masuala ya usajili wa laini za simu yameainishwa katika Kanuni za Usajili wa laini za simu za mwaka 2020 (The Electronic and Postal Communications SIM Card Registration).

Kwa mujibu wa kanuni hizo, ambazo Mwananchi imeziona kifungu cha 18(1) kinasema, ‘Mtu anayekusudia kumiliki na kutumia kadi ya SIM ya simu ya mkononi iliyomo ndani ya simu au kadi ya kuchomeka kwenye kifaa cha mawasiliano, atatakiwa kusajili (a) kama ni mtu mmoja, si zaidi ya laini moja kwa kila mtandao mmoja wenye leseni kwa matumizi ya kupiga simu, kutuma ujumbe na matumizi ya intaneti.