Anti Bettie: Anatumia muda mrefu kumaliza, nafikiria kuachana naye

Anatumia muda mrefu kumaliza, nafikiria kuachana naye

Muktasari:

  • Tulikuwa wapenzi kwa mwezi mmoja akaniposa, hivyo mwanzoni nilijua ni ugeni akinizoea atakuwa sawa, lakini hali haibadiliki.

Nina mchumba ambaye tunatarajia kufunga ndoa mwishoni mwa mwaka huu.

Kwa kweli namshukuru Mungu ananitimizia kila kitu na ana mapenzi kwangu, ndugu na marafiki zangu. Tatizo moja na ninalohisi ananishinda ni kuchelewa kumaliza tunapokuwa faragha.

Kuna wakati natamani kuvunja uchumba, nahisi huko mbele atanishinda. Tulikuwa wapenzi kwa mwezi mmoja akaniposa, hivyo mwanzoni nilijua ni ugeni akinizoea atakuwa sawa, lakini hali haibadiliki.

Hakika ninatamani kuvunja uchumba, nishauri nifanyeje?

Haaahaaa usinichekeshe, uvunje uchumba kwa mtu anayekupenda na kukujali kwa sababu ya shughuli za faragha, hebu kaa kwa kutulia kwanza.

Sikiliza, haachwi mwanamke kwa sababu ya kushindwa kumhudumia bwana, ondoa hilo wazo na endelea na mipango ya harusi kama kawaida.

Jambo la kwanza unalopaswa kufanya ni kumsoma maeneo ambayo ukimshika anachanganyikiwa au kujua vitu ambavyo ukifanya mkiwa faragha vinamvuruga na kumaliza.

Unaweza kumsoma wewe mwenyewe au kwa kumuuliza anapenda ufanye nini, umshike wapi. Ila ukimsoma wewe utafaidika zaidi kuliko akikuambia atakuwa mjanja hakupi nafasi ya kuyashika.

Pili, tumia muda mwingi kucheza naye kwa kufanya hiki na kile, kumshika huku na kule kabla hamjaingia katika tukio husika ili umchoshe kwanza. Hapa panahitaji ujuzi, uwezo wa kutumia muda kwingi kufanya hivyo bila kuchoka napo pia panahitaji walau ujue anapenda kufanyiwa nini ili asiboreke, badala yake afurahie utalii wa mikono na mwili wako mwilini mwake.

Kwa kifupi usimpe nafasi ya kutawala mchezo kuanzia mwanzo hadi mwisho, ukitulia na kusubiri kila kitu akufanyie anaingia kwenye gemu akiwa timamu anavurugika kadri mchezo unavyoendelea na ndiyo maana anachukua muda mwingi kumaliza.

Mbinu hizo zikishindwa mweleze mapema namna kuchelewa kwake kunavyokupa mashaka huko mbele ya safari kama utammudu, jadilianeni kwa pamoja nini cha kufanya.

Hapa napo hutakiwi kwenda kuzungumza naye kama mnajadili kununua nyumba au gari, yaani ukiwa katika hali ya kawaida, unapaswa utumie uanamke wako ujilainishe na utumie sauti ya mahaba ili muelewane, jambo la mapenzi hujadiliwa kimapenzi.

Wewe pia saikolojia yako ibadilishe, kabla ya kuingia faraghani hakikisha upo tayari kwa ajili ya tukio hilo, ukiiweka akili yako ananichosha ananichosha utachoka kweli na wasiochoka watapita naye.

Wakati mwingine mapenzi ni namna unavyoyachukulia, kila siku ukilalamika unaumia hutakaa uyafurahie kamwe, akili yako iambie mapenzi ni raha. Tena isumbue kujiuliza kwa nini mchumba wangu anishinde mimi mtoto wa kike, jipe moyo unamuweza na amua kufanya hivyo.

Usikubali kushindwa, tembo asiyekuwa na akili ya kupambanua mambo hashindwi na mkonga wake, sembuse wewe tena mwanamke! Sitarajii ushindwe.