Anusurika kifo baada ya kujikata uume kwa wivu wa mapenzi

Anusurika kifo baada ya kujikata uume kwa wivu wa mapenzi

Muktasari:

  • Majirani wa Tarimo aliyetaka kujiua wamesema kuwa jirani yao alikuwa na ugomvi na mkewe wa muda mrefu.

Arusha. Mkazi Kijenge Mwanama jijini Arusha, John Tarimo amelazwa katika hospitali ya mkoa Arusha ya Mount Meru baada ya kujikata uume na kutaka kujiua kutokana na ugomvi wa mapenzi.

Wakizungumza na Mwananchi Leo Januari 25, baadhi ya majirani walioshuhudia tukio hilo wamesema walimkuta Tarimo akiwa hajitambui.

Onesmo Mjema amesema Tarimo alikuwa amejifungia ndani ya chumba alichokiwa amepanga akiwa ameukata uume na kubaki sehemu ndogo na amejikata mkono huku akitoka mapovu mdomoni.

"Mke wake alikuwa ametoka amemuacha ndani lakini aliporudi akiwa mtoto wao mmoja alikuta mlango umefungwa ndipo baada ya kuchungulia dirishani alikuona mumewe akiwa ametapakaa damu na anatoka mapovu," amesema Mjema.

Ameendelea kusema akiwa na jirani mwingine walivunja mlango na kuingia ndani kumtoa nje akiwa hawezi kuzungumza huku damu zikimtoka.

"Baada ya hapo tulimwita mwenyekiti wa mtaa ambaye alitupa maelekezo tumpeleke hospitali kuokoa maisha," amesema.

Kamanda wa Polisi mkoa Arusha, Salum Hamduni amethibitisha kutokea tukio hilo na kueleza kijana huyo yupo chini ya ulinzi wa Polisi.

"Ingawa anapata matibabu lakini yupo chini ya uangalizi wa Polisi na anatuhumiwa kwa kutaka kujiua," amesema Kamanda Hamduni.

Taarifa za awali zinadai kuwa mtuhumiwa huyo aliacha ujumbe  kuwa anajiua kutokana na ugomvi kati ya mke wake na ndugu zake bila ya kufafanua.

Hata hivyo, mmoja wa majirani aliyeomba kuhifadhiwa jina lake amesema kwa muda mrefu kulikuwa na ugomvi  wa wivu wa mapenzi baina ya Tarimo  na mkewe ambaye wamezaa nae mtoto mmoja.