Auawa kwa kukatwa mapanga na watu wasiojulikana
Muktasari:
- Sikujua Maghembe, mkazi wa kitongoji cha Nyakitono kijiji cha Makundusi Wilaya ya Serengeti ameuawa baada ya kuvamiwa nyumbani kwake na kukatwa mapanga.
Serengeti. Sikujua Maghembe, mkazi wa kitongoji cha Nyakitono kijiji cha Makundusi Wilaya ya Serengeti ameuawa baada ya kuvamiwa nyumbani kwake na kukatwa mapanga.
Akizungunza leo Alhamisi Oktoba 7,2021 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Longinus Tibishibwamu amesema mauaji hayo yametokea jana Jumatano Oktoba 6,2021
"Haya ni mauaji ya kupanga maana watuhumiwa hawakuchukua kitu bali wamemkatakata sehemu mbalimbali za mwili kisha wakatokomea,tunaendelea na uchunguzi kubaini undani wake kisha tutatoa taarifa zaidi," amesema.
Mwenyekiti wa Serikali ya kijiji hicho, Joseph Nyaikobe ameieleza Mwananchi Digital kuwa watoto wanadai wakati wamekaa kwenye korido ghafla waliingia watu watatu wakiwa na tochi zenye mwanga mkali wakamulika na kuanza kumshambulia huyo mama.
"Alikuwa amekaa na mwanaume ambaye anaishi naye baada ya mme wake kufariki mwaka jana,ambaye ni fundi lakini katokea huko Bariadi ambaye alipigwa ubapa wa panga akakimbia na kuanza kumkatakata na kusababishia kifo chake pale pale," amesema.
Amesema hilo tukio limeacha maswali mengi kwa kuwa mara nyingi matukio kama hayo huambatana na wizi hasa mifugo lakini hao hawakuchukua kitu.