Bashe amjibu Mpina

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe akizungumza bungeni alipokuwa ajibu hoja za wabunge waliochangia mjadala wa kupitisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2022/2023, jijini Dar es Salaam leo. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

Wakati Mbunge wa Kisesa (CCM), Luhaga Mpina akisema kupanda kwa bei za mbolea kumetokana na Serikali kufuta mfumo wa uagizaji wa mbolea kwa pamoja ,Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amesema ni hatari kwa mtu aliyewahi kuwa waziri na mbunge wa muda mrefu kuupotosha umma.

Dodoma. Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe amemcharukia Waziri wa zamani wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina ambapo amesema ni hatari kwa mbunge wa muda mrefu kuupotosha umma.

Mpina wakati akichangia mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka 2022/2023 bungeni leo Jumatano Mei 18, 2022 amesema bei ya mbolea imeanza kupanda kabla ya vita vya Ukraine na Russia.

Akichangia makadirio hayo, Mpina alisema bei za mbolea zilianza kupanda baada ya Serikali kuondoa utaratibu wa ununuzi wa mbolea kwa pamoja ili kufanikisha njama za wafanyabiashara wachache waliokuwa wamepanga kuja kuwaongezea wakulima bei za mbolea.

Mpina akichangia Bajeti ya Kilimo

Amesema bei za mbolea zilianza kupanda kwa kasi baada ya Serikali kuondoa mfumo huo mwaka 2021 na wala si baada ya vita ya Ukraine na Russia.

Akijibu hoja za wabunge, Bashe amesema ni hatari kwa mtu ambaye amekuwa waziri, naibu waziri na mbunge wa muda mrefu kusimamia bungeni na kutoa mada ambayo inapotosha umma.

Amesema bei ya mbolea duniani si jambo la kuficha ni kama bidhaa nyingine hata ukigoogle unapata bei za mbolea duniani.

Amesema Machi mwaka 2018 mbolea aina ya DP ilikuwa ni Dola za Marekani 549 lakini hivi sasa ni Dola za Marekani 948.

Amesema mbolea ya Urea iliyokuwa ikiuzwa Dola za Marekani 134 sasa hivi ni Dola za Marekani 723.

“Hili sio jambo la siri halifichwi liko wazi. Kama ana source (chanzo ya kuleta) ya kuleta mbolea nchini kwa bei ya rahisi amletee atasaini kwa ajili ya kuleta tani zote 400,000,”amesema.

Amesema wasipotoa ruzuku ya mbolea watakuwa wanawaonea, kuwaumiza na hawawatendei haki wakulima bali wanawaumiza.

 “Tutakuwa hatutakii Taifa letu uhai, tusifanye siasa kwenye mambo hatari, hiii siasa ndio imeua kitalu cha pamba katika jimbo lale (Kisesa),”amesema.

Amesema kuwa Serikali inafufua Kampuni ya Mbolea Nchini (TFC) na imeipatia Sh6 bilioni kwa ajili ya kwenda kununua mbolea nje ya nchi na kushindana na waagizaji wengine wa mbolea.