Bawacha wadai kukamatwa wakifanya mazoezi

Bawacha wadai kukamatwa wakifanya mazoezi

Muktasari:

  •  Wanachama na wafuasi wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha) waliokuwa wanafanya mazoezi ya kukumbia (jogging) katika viwanja vya Tanganyika Packres jijini Dar es Salaam wanadaiwa kushikiliwa na jeshi la polisi katika kituo cha Wazo.


Dar es Salaam. Wanachama na wafuasi wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha) waliokuwa wanafanya mazoezi ya kukumbia (jogging) katika viwanja vya Tanganyika Packres jijini Dar es Salaam wanadaiwa kushikiliwa na jeshi la polisi katika kituo cha Wazo.

Akizungumza na Mwananchi Digital leo Jumamosi Oktoba 2,2021 Mjumbe wa Sekretarieti, Habari na Mawasiliano Bawacha Devotha Minja amesema, wanawake hao wamekamatwa wakakati wanafanya mazoezi katika viwanja vya Tanganyika Packres Kawe.

Ingawa Minja hakuweka wazi sababu za kukamatwa kwa wenzao lakini taarifa zilizoenea kukamatwa kwao kunatokana na kutokuwa na kibali cha kukusanyika kinachotolewa na polisi wa eneo husika.

Hata hivyo Minja amesema lengo la mazoezi hayo, ni kuhamasisha wanawake kufanya mazoezi kila Jumamosi ili kujilinda na maradhi mbalimbali ikiwemo Uviko 19.

“Ilikuwa asubuhi wakati wanafanya mazoezi, polisi walifika wakiwa na magari mawili na kuanza kuwakamata bila taarifa yoyote, wamepelekwa kituo cha polisi Wazo ingawa hadi sasa hatujafahamu idadi kamili ya waliokamatwa,”amesema Minja.

 “Zoezi hili tumelianza mwezi mmoja uliopita, na tunaendelea kuwahamasisha wanawake nchi nzima kufanya mazoezi, lakini hatujui kwanini polisi wamekuwa wanaingilia na kutuzuia tusifanye mazoezi,”amesema.

Alipotafutwa Kamanda wa Polisi mkoa wa Kinondoni Ramadhani Kingai, hakutaka kuzungumza na kutaka atafutwe Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar Saalaam, Jumanne Muliro.

Hata hivyo Kamanda Muliro alipotafutwa na Mwananchi Digital, hakupatikana kutokana na simu zake za mkononi kutokuwa hewani.