Benki ya Damu Salama yasema bado kuna changamoto ya upatikanaji wa damu

Benki ya Damu Salama yasema bado kuna changamoto ya upatikanaji wa damu

Muktasari:

  • Benki ya Damu Salama Tanzania imeadhimisha kumbukumbu ya miaka 22 ya kifo cha Mwalimu Julius Nyerere ikiwahimisha Watanzania kuchangia damu.

Dodoma. Benki ya Damu Salama Tanzani imesema bado kuna upungufu mkubwa wa damu nchini na kuwataka wadau kujitokeza kuchangia ili kuokoa maisha ya wagonjwa.

Hayo yameelezwa leo Alhamisi Oktoba 14, 2021 na Msimamizi wa kituo cha kanda, Dk Leah Kitundu wakati wa maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 22 tangu kifo cha Hayati Mwalimu Julius Nyerere yaliyofanyika mkoani hapa.

Dk Leah amesema wakati mahitaji ya damu kwa mwezi mkoani humo ni kati ya chupa 1000 hadi 1500, lakini kiasi kinachokusanywa ni chupa 800 hadi 900.

“Kwa kawaida damu ina muda wake wa kuishi ni siku 35 pia haijawahi kutokea damu kumwagwa, inatumika na kuisha,” amesema.

Katika maadhimisho hayo, Jumuiya ya Tulakhlaaqul Islaam (JAI), ilichangia damu katika benki hiyo, huku Taasisi Tanzania Patriotic Organization (TPO) ikifanya usafi katika Hospitali ya Rufaa ya Dodoma.

Akizungumza mara baada ya kufanya usafi, Mwenyekiti wa TPO Kasmir John amewataka vijana kujitoa ili kufanikisha mambo ambayo Mwalimu Nyerere aliwaachia ikiwemo umoja na mshikamano.

“Wito wetu kwa jamii ni namna ya kujitoa kufanya shughuli za kijamii kwa kufanya hivyo ni moja ya kumuenzi Baba wa Taifa kwa tufanya Watanzania sote kuwa wamoja na wenye mshikamano,” amesema.

Mratibu Mkuu JAI Taifa Athumani Massanga amesema wameamua kumuenzi Mwalimu Nyerere kwa kuchangia damu kwasababu kitendo hicho ni moja ya ibada.

 “JAI imekuwa ikijipambanua kama jumuiya ya tabia njema za Kiislaam kwa misingi ya kuwasaidia watu wote wenye mahitaji bila kujali itikadi za kidini, ukabila, itikadi za kisiasa wala mzawa,” amesema.