Bosi TRA akataa ombi la wafanyabiashara kuhusu EFD

New Content Item (1)
Bosi TRA akataa ombi la wafanyabiashara kuhusu EFD

Muktasari:

Wafanyabiashara jijini Arusha wameiomba Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuongeza muda wa kuboresha mashine za kielektroniki za kutoa risiti (EFD) kwa madai kuwa muda wa mwezi mmoja uliowekwa ni mfupi.

Arusha. Wafanyabiashara jijini Arusha wameiomba Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuongeza muda wa kuboresha mashine za kielektroniki za kutoa risiti (EFD) kwa madai kuwa muda wa mwezi mmoja uliowekwa ni mfupi.

Wakizungumza leo Jumatano Januari 13, 2020  mmoja wa wafanyabiashara hao, Alfayo Kimaro amesema muda wa mwezi mmoja waliopewa kuboresha mashine hiyo ni mfupi na kuomba uongezwe.

“Tungependa Serikali ituongezee muda kwani wengi hatukuwa na elimu juu mashine hizo,  pia tunahitaji elimu namna ya kuweza kupata mashine hizo pamoja na matumizi" amesema

Kamishna mkuu wa TRA, Dk Edwin Mhede amesema mamlaka hiyo haiongezi muda wa kuboresha mashine badala yake itachukua hatua za kisheria kwa ambao hawataboresha.

Ameeleza hayo wakati akifungua mkutano mkuu wa nusu mwaka wa mamlaka hiyo ambapo  alipokea ombi la muda kuongezwa muda na kubainisha kuwa jambo hilo halitawezekana kwa kuwa muda waliopewa wafanyabiashara kuanzia Desemba 7, 2020 hadi Januari 7, 2021 ulikuwa mrefu na wangeweza kukamilisha kila kitu.

“...,maboresho ni lazima yaendane na aina ya mashine tunazozitumia hivi sasa na  upatikanaji wake ni wa dakika chache kwa hiyo nasema kuongeza muda ni jambo ambalo haliwezekani inajulikana wazi kuwa utiifu wakati mwingine lazima watu walazimishwe,” amesema