Chadema yasema haipo tayari kukutanishwa na Polisi

Mkurugenzi wa Itikadi, Uenezi na Mambo ya Nje wa Chadema, John Mrema.

Muktasari:

  • Chadema wamesema hawapo tayari kukutanishwa na jeshi la polisi, kama ambavyo ametangaza Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi ili kuondoa mvutano kati yao na  vyama vya siasa na jeshi hilo.

Dar es Salaam. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema hakipo tayari kukutanishwa na jeshi la polisi, kama ambavyo ametangaza Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi ili kuondoa mvutano kati yao, vyama vya siasa na jeshi hilo.

Hayo yamesemwa leo Jumanne Septemba, 7,2021  na Mkurugenzi wa Itikadi, Uenezi na Mambo ya Nje wa Chadema, John Mrema alipozungumza na waandishi wa habari.

Mrema amesema hawaoni haja ya kukutanishwa na jeshi hilo kwa kuwa kwa mambo ambayo wamekuwa wakiyafanya kwa miaka sita amedai ni wahalifu ambao wangetakiwa wawe wameshafikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Badala yake amesema Chadema itaendelea na taratibu zake za ufanyaji vikao kama katiba inavyowaruhusu, lakini suala la kukutanishwa na Jeshi la Polisi hawapo tayari.

"Jana msajili wa vyama vya siasa amesema atakutanisha vyama vya siasa na Jeshi la Polisi, msimamo wetu Chadema ni kwamba hatupo tayari kushiriki mkutano huo," amesema Mrema.