DPP amewafutia kesi waliodaiwa kusafirisha wenye ulemavu, kuwatumikisha

What you need to know:

  • Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewafutia kesi na kuwaachia huru washtakiwa 14 waliokuwa wanakabiliwa na mashtaka 41 yakiwemo ya kufanya biashara haramu ya kusafirisha binadamu, kukwepa kodi na kuisababishia hasara ya Sh31 milioni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewafutia kesi na kuwaachia huru washtakiwa 14 waliokuwa wanakabiliwa na mashtaka 41 yakiwemo ya kufanya biashara haramu ya kusafirisha binadamu, kukwepa kodi na kuisababishia hasara ya Sh31 milioni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Wameachiwa baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini Tanzania (DPP) kuwasilisha hati mahakamani akieleza kuwa hana nia ya kuendelea na shauri hilo.

Washtakiwa hao walidaiwa kusafirisha walemavu 37 wakiwemo watoto wadogo wenye umri wa miaka saba na 11 kutoka Mikoa ya Tabora, Shinyanga na kuwaleta Dar es Salaam na kuwafanya kuwa ombaomba mitaani kwa lengo la kujiingizia kipato.

Uamuzi wa kuwafutia kesi na kuwaachia huru umetolewa leo Jumanne Juni 22, 2021 na hakimu mkazi mwandamizi, Kassian Matembele wakati kesi hiyo ilipoitwa kwa ajili ya kutajwa.

Awali, wakili wa Serikali mwandamizi, Wankyo Simon amedai kuwa DPP ameieleza mahakama kuwa hana nia ya kuendelea na shauri hilo.

Wakili huyo amedai washtakiwa hao wamefutiwa mashtaka chini ya kifungu namba 91(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai  ( CPA) sura ya 20 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2019.

Baada ya upande mashtaka kueleza hiyo, hakimu alikubaliana na ombi hilo na kuwafutia mashtaka na kisha kuwaachia huru.

Waliofutiwa mashtaka ni katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 2/2021 ni Yusuph Mbuani, Joseph Magafu, Emmanuel Salu, Gogad Mayenga, Samson Akunahai, Husein John,  Zacharias Paul, Dotto Shigula, Petro Simon, Emmanuel Sahani, Joseph Mathias, Massanja Paul, Aminiel Sangu na Emmanuel Lusinge.

Kati ya mashtaka hayo 41 moja ni la kuongoza genge la uhalifu, mashtaka  37 ni ya kusafirisha na kutumikisha walemavu katika biashara ya kuomba barabarani.

Mashtaka mengine waliyofutiwa ni kukwepa kodi, kuisababishia hasara TRA na kutakatisha Sh31 milioni.



This page might use cookies if your analytics vendor requires them.