Eneo la Mlima Kenya kuamua urais Kenya

Muktasari:

Zikiwa zimesalia siku saba kufanyika kwa uchaguzi mkuu wa Rais nchini Kenya, kampeni zimezidi kupamba moto huku eneo la Mlima Kenya likipewa nafasi zaidi ya kuamua mshindi katika uchaguzi huo.

Kirinyaga, Kenya. Zikiwa zimesalia siku saba kufanyika kwa uchaguzi mkuu wa Rais nchini Kenya, kampeni zimezidi kupamba moto huku eneo la Mlima Kenya likipewa nafasi zaidi ya kuamua mshindi katika uchaguzi huo.

Helikopta inatua katikati ya mashamba ya mpunga, ikiashiria kuwasili kwa mgombea urais wa Kenya, William Ruto akitafuta kura katika eneo la Mlima Kenya lenye watu wengi na lenye ushawishi mkubwa kisiasa.

Likiwa katikati mwa nchi na kuzungukwa na volcano iliyotoweka inayoipa eneo hilo jina lake, Mlima Kenya imekuwa na jukumu muhimu katika uchaguzi wa urais kwa muda mrefu na mwaka huu pia.

Ruto anaonekana bado mchanga kwenye uchaguzi wa Agosti 9 ambapo atapambana na Raila Odinga, mwanasiasa mkongwe wa upinzani ambaye sasa anaungwa mkono na chama tawala cha Jubilee, Ruto na timu yake wanajua kwamba kushinda Mlima Kenya ni muhimu.

Mgombea huyo mwenye umri wa miaka 55 ameapa kuwainua mamilioni ya Wakenya kutoka kwenye umaskini na amefanya ukuaji wa uchumi “kuanzia chini kwenda juu” kuwa nguzo kuu ya kampeni yake.

Katika mkutano huo wa kampeni uliofanyika Kirinyaga, Nancy Njeri, mkulima wa mpunga mwenye umri wa miaka 78, aliiambia AFP kuwa tayari anajua wa kumpa kura yake.

“Ruto ataleta mabadiliko katika elimu, ajira kwa vijana, atahakikisha tuna mbolea ya kukuza mpunga wetu, na mambo mengine mengi,” alisema.

Gavana wa Kirinyaga, Anne Waiguru alitabiri ushindi mkubwa kwa chama cha Ruto cha United Democratic Alliance (UDA) katika eneo hilo, akiambia AFP kwamba yeye ni “mtu anayekubalika na watu wa Mlima Kenya.”

“Amefanya mambo mengi ya msingi katika suala hilo,” mwanasiasa huyo wa UDA alisema.

Ruto, mfanyabiashara kutoka kabila la Wakalenjin ambaye kwa sasa anahudumu kama Naibu wa Rais wa Kenya, awali alipangiwa kumrithi Rais Uhuru Kenyatta.

Badala yake, alijikuta akiwekwa pembeni baada ya bosi wake kufikia makubaliano na mpinzani mkuu, Odinga.

Akiwa na uchungu lakini mwenye malengo, Ruto alizindua chama kipya na kuanza kuweka msingi wa kuwania urais, akilenga hasa eneo ambalo labda linawakilisha zaidi siasa tata zinazotawala Kenya.

Ilikuwa ni jambo kubwa kwa kiongozi wa Wakalenjin, angalau atakuwa kwenye karatasi ya kura.

Mlima Kenya ni ardhi takatifu ya Wakikuyu, kabila kubwa zaidi la Kenya, wanaoamini kwamba Mungu anaishi katika volkano yenye theluji wanayoiita Kirinyaga.

Eneo lenye rutuba ambalo ni nyumbani kwa bustani za miembe na mashamba ya kahawa, pia linachukua nafasi takatifu katika historia ya Kenya, uasi wa Mau Mau dhidi ya Milki ya Uingereza ulianzia huko mwaka wa 1952.

“Kuanzia wakati huo (na kuendelea) kuna hisia hii ya haki ambayo Wakikuyu wamekuwa nayo kila wakati,” anasema mchambuzi, Herman Manyora ambaye anampenda Odinga.

Takriban miongo sita baada ya uhuru mwaka wa 1963, Mlima Kenya unaendelea kuwa kiini cha siasa za Kenya.

Marais watatu kati ya wanne wa Kenya, Jomo Kenyatta, mwanaye Uhuru na Mwai Kibaki ni Wakikuyu.

Hata hivyo, mwaka huu, Wakikuyu ambao wanatoa takriban wapigakura milioni sita kati ya milioni 22 wa Kenya, watalazimika kuchagua kati ya Ruto, Mkalenjin na Odinga, Mjaluo.