EU yatoa Sh44.3 bilioni kwa kaya masikini Tanzania

Muktasari:

  • Tanzania imepokea msaada wa Sh44.3 bilioni kwa ajili ya mpango wa kunusuru kaya maskini awamu ya pili (PSSN II).

Dar es Salaam. Tanzania imepokea msaada wa Sh44.3 bilioni kwa ajili ya mpango wa kunusuru kaya maskini awamu ya pili (PSSN II).


Hafla ya kusainiwa kwa mkataba huo imefanyika leo Alhamisi Juni 16, 2022 kati ya Serikali ya Tanzania na Sweden  zilizotolewa na Umoja wa Ulaya (EU) ambazo ni sawa na Euro milioni 18.7 zitakazosimamiwa na ubalozi wa Sweden.


Katibu mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Emmanuel Tutuba amesema msaada huo  utasaidia kupunguza upungufu wa fedha kwa ajili ya programu hiyo.

“Kwa niaba ya Serikali natoa shukran za dhati kwa EU kwa msaada huu muhimu na wamejua PSSN inachangia kwa ukubwa sana kupunguza umaskini uliokithiri kwa watu wa Tanzania."

“Lengo la ufadhili huu ni kuwezesha PSSN kuboresha hali za uchumi ya wanawake kwa kufadhili familia masikini kuwawezesha kupata fursa za kuongeza kipato na huduma za kiuchumi na za kijamii,” amesema Tutuba.

Mkuu wa ushirikiano wa kimaendeleo wa umoja wa Ulaya nchini Tanzania, Cedric Merel amesema wataendelea kushirikiana kwa pamoja ili kuleta maendeleo chanya kwa kundi la watoto na wanawake nchini Tanzania.


“Hili ni kundi lengwa la Tasaf na kubwa tunaangalia ni namna gani tutapunguza suala ukatili wa kijinsia, ni kwamba ukitaka kutekeleza uhifadhi wa jamii kikamilifu, ukiwekeza kwa wanawake unakuwa ni mkakati utakaofanikiwa,” amesema Cedric.

Mkuu wa ushirikiano wa maendeleo kutoka ubalozi wa Sweden nchini Tanzania, Sandra Diesel amesema wanatarajia kuongeza ufadhili zaidi siku za mbeleni ili kuzidi kupunguza upungufu wa kifedha uliopo kwa ajili ya utekelezaji wa programu ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Mbali na fedha za msaada za mkataba uliosainiwa leo, Serikali ya Sweden imekuwa ikisaidia mpango huo tangu mwaka 2015 ambapo ilitoa SEK milioni 750 sawa na dola za Marekani(USD) milioni 86 kwa awamu ya kwanza ya programu ikifuatiwa na SEK milioni 550 sawa na USD milioni 63.