Hawa ndiyo vinara kumi matokeo mtihani darasa la Saba mwaka 2020

Angalia hapa matokeo ya Darasa la Saba

Muktasari:

Watahiniwa bora kitaifa wa mtihani wa kumaliza elimu ya msingi ni wale ambao wamepata alama nyingi zaidi kuliko wenzao kwenye masomo matano waliyotahiniwa.

Dar es Salaam. Baraza la Mitihani la Taifa nchini Tanzania (Necta), limemtaja mwanafunzi aliyehitimu shule ya msingi Graiyaki iliyopo mkoani Mara, Herrieth Japhet Josephat kuwa ndiye aliyeibuka kinara katika matokeo ya mtihani wa kuhitimu  elimu ya msingi (Psle).

Herrieth anakuwa msichana pekee kati ya watahiniwa 10 bora kitaifa, waliotajwa na baraza leo Jumamosi, Novemba 21, 2020 wakati Katibu Mtendaji wa Necta, Dk Charles Msonde akitoa taarifa ya matokeo hayo.

“Watahiniwa hawa bora kitaifa ni wale ambao wamepata alama nyingi zaidi kuliko wenzao kwenye masomo matano waliyotahiniwa, ambapo pia kuna mchanganuo kwa wasichana 10 bora, wavulana 10 bora,” alisema Dk Msonde.

Alimtaja aliyeshika nafasi ya pili kuwa ni Huma Masala Huma kutoka shule ya msingi Kwema Morden ya Shinyanga na nafasi ya tatu ikienda kwa Gregory Mtete Alphonce kutoka Twibhoki shule ya msingi iliyopo mkoani Mara.

Aliyeshika nafasi ya nne ni Nyambina Musa Nyambina kutoka shule ya msingi Graiyaki iliyopo Mara pia.

Andrew Elias Mabula kutoka shule ya msingi Kwema Morden ya Shinganya, ameshika nafasi ya tano, Jonas Nyamataga Ayubu (Little Flower) Mara, Emmanuel Kashinje Paul (Kwema Morden) Shinyanga, Emmanuel Peter Marwa (Kwema Morden) Shinyanga, Prosper Aspenas Tumbo (God’s Bridge) Mbeya na nafasi ya 10 ilikwenda kwa Yesaya Mnkondo Bendera kutoka shule ya msingi God’s Bridge ya jijini Mbeya.