HESLB: Wanafunzi 782 kupata mikopo asilimia 100

HESLB: Wanafunzi 782 kupata mikopo asilimia 100

Muktasari:

  • Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetangaza orodha ya wanafunzi 782 watakaopata mikopo asilimia 100 bila kujali masomo waliyochaguliwa kujiunga.


Dodoma. Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetangaza orodha ya wanafunzi 782 watakaopata mikopo asilimia 100 bila kujali masomo waliyochaguliwa kujiunga.

Idadi hiyo ni kwa waombaji waliothibitishwa kuwa wanatoka kaya masikini ambazo zinahudumiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf).

Kauli hiyo imetolewa leo Jumatano Septemba 15, 2021 na mkurugenzi mtendaji wa bodi hiyo, Abdul-Razaq Badru wakati wa utiaji saini makubaliano ya kutoa mkopo kwa waombaji kutoka kaya masikini.

Badru amesema wanafunzi hao watapata mikopo kabla ya kuanza masomo ili kuwapunguzia usumbufu.

Amesema mpango huo ni endelevu na tayari wameweka utaratibu wa kuwafuatilia kuanzia shule za msingi hadi kidato cha sita.

"Tumeandaa mfumo wa pamoja na wenzetu Wizara ya Elimu na Tasaf, tutakuwa tukiwabaini wanafunzi mapema hivyo uombaji wao utakuwa na kipaumbele chake," amesema Badru.

Kuhusu waombaji wengine amesema dirisha limefungwa.