Hospitali, vituo vya afya Manyara vyakabidhiwa vifaa vya Sh10.2 milioni

Muktasari:

  • Mdau wa maendeleo wa Mkoa wa Manyara, Emmanuel Khambay amekabidhi msaada wa vifaa mbalimbali vya thamani ya Sh10.2 milioni katika hospitali ya Mji wa Babati (Mrara), vituo vitatu vya afya na zahanati mbili.

Mdau wa maendeleo wa Mkoa wa Manyara, Emmanuel Khambay amekabidhi msaada wa vifaa mbalimbali vya thamani ya Sh10.2 milioni katika hospitali ya Mji wa Babati (Mrara), vituo vitatu vya afya na zahanati mbili.

Msaada huo umehusisha meza za kuhifadhi dawa, vyakula vya wagonjwa, mabenchi ya kukalia wagonjwa na viti vya kukalia manesi na madaktari.

Khambay akizungumza na Mwananchi Digital leo Aprili 26 amesema ametoa msaada huo baada ya kuguswa aliposikia kuna changamoto ya vifaa hivyo.

Amesema vifaa hivyo vitatolewa katika hospitali ya Mrara ya mji wa Babati, vituo vya afya Mutuka, Singe, Bonga na zahanati za Nakwa na Malangi.

"Baada ya viongozi wa UVCCM mji wa Babati wakiongozwa na Mwenyekiti, Hassan Mdinku na Katibu Hamasa, Idd Sulle kusema changamoto hizo nilitoa kidogo nilichonacho ili kupungua changamoto hizo," amesema Khambay.

Mkuu wa Wilaya ya Babati, Lazaro Twange amewapongeza UVCCM Babati mjini kwa kuwa wabunifu na kutafuta wadau kama Khambay wanaoweza kumaliza au kupunguza changamoto.