Idadi ya vifo ajali ya Mtwara yafikia 13


Muktasari:

Idadi ya waliofariki dunia katika ajali ya ya gari la Shule ya King David iliyotokea katika eneo la Mjimwema, Kata ya Mikindani, Mtwara Mjini imefika 13 baada ya wanafunzi wengine wawili kufariki dunia.

Mtwara. Idadi ya waliofariki dunia katika ajali ya ya gari la Shule ya King David iliyotokea katika eneo la Mjimwema, Kata ya Mikindani, Mtwara Mjini imefika 13 baada ya wanafunzi wengine wawili kufariki dunia.

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Brigedia Jenerali Marco Gaguti amesema majeruhi wawili wamefariki dunia wakipatiwa matibabu Hospitali ya Ligula na kufanya jumla ya waliofariki dunia kuwa 13.

Ajali hiyo ambayo ilitokea leo Jumanne Julai 26, 2022 asubuhi katika eneo la Mjimwema, Kata ya Mikindani, Mtwara Mjini imesababisa vifo vya watu 13 wakiwamo watoto wawili wa familia moja.

Hata hivyo, mwanafunzi mmoja alifafiki dunia wakati akipatiwa matibabu na baadaye Mkuu huyo wa Mkoa ametoa taarifa kuwa wengine wawili wamefariki dunia.

Gaguti amesema majeruhi watano wamehamishiwa Hospitali ya Rufaa ya Ndanda kuendelea na matibabu.

Awali, akizungumzia chanzo cha ajali hiyo, Kaimu Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara, Nicodemus Katembo alisema ni gari kufeli kwa breki kisha kutumbukia shimoni.

Katembo amesema gari hiyo aina ya Hiace ilifeli breki na kumshinda dereva kisha kuingia kwenye mteremko.