IGP Wambura afanya mabadiliko makamanda wa Polisi

Muktasari:

  • Katika mabadiliko hayo aliyekuwa kamanda wa polisi mkoa wa kipolisi Temeke ACP Richard Ngole amehamishiwa makao makuu ya polisi Dodoma.

Dar es Salaam. Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Camilius Wambura amewahamisha mikoa ya kazi baadhi ya makamanda wa polisi huku mmoja akirudishwa makao makuu Dodoma.

Taarifa iliyotolewa leo Jumanne Septemba 20, 2022 na msemaji wa Jeshi la Polisi, David Misime imeeleza kuwa, waliohamishwa ni Kamishna msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Henry Mwaibambe kutoka mkoa wa Geita kwenda mkoa wa Tanga.

Aliyekuwa kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Safia Shomary amehamishiwa mkoa wa Geita kuchukua nafasi ya Kamanda Mwaibambe.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa, aliyekuwa Kamanda wa Polisi mkoa wa kipolisi Temeke ACP Richard Ngole amehamishiwa makao makuu ya jeshi hilo mkoani Dodoma.

Nafasi ya Ngole yinachukuliwa na ACP Kungu Malulu ambaye alikuwa kamanda wa polisi mkoa wa kipolisi Rufiji.