Jafo aitaka Nemc kufuatilia matumizi ya vifungashio visivyokidhi ubora

Jafo aitaka Nemc kufuatilia matumizi ya vifungashio visivyokidhi ubora

Muktasari:

  • Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (muungano na mazingira), Seleman Jafo ameliagiza Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira nchini Tanzania (Nemc) kuanzia kesho Ijumaa Aprili 9, 2021 kufuatilia matumizi ya vifungashio vya plastiki visivyokidhi viwango vya ubora.

Dodoma. Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (muungano na mazingira), Seleman Jafo ameliagiza Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira nchini Tanzania (Nemc) kuanzia kesho Ijumaa Aprili 9, 2021 kufuatilia matumizi ya vifungashio vya plastiki visivyokidhi viwango vya ubora.

Leo ni siku ya mwisho iliyotangazwa na Serikali kwa kutumika kwa vifungashio visivyokidhi vigezo vya ubora vya Shirika la Viwango Tanzania (TBS).

Akizungumza leo Alhamisi Aprili 8, 2021 wakati akikagua kiwanda cha plastiki cha Future Colourful Ltd kilichopo Kizota jijini Dodoma, Jafo amesema

mwisho ya matumizi ya vifungashio visivyoruhusiwa ni leo akisisitiza kuwa elimu imetolewa kwa muda mrefu kuwezesha mabadiliko yanayofuata sheria.

“Nimeshatoa maelekezo nimewaelekeza watu wetu wa Nemc kuanzia kesho kufuata ufuatiliaji wa vifungashio vyote ambavyo viko katika katazo,” amesema.

Amesema kwa watu wanaofanya biashara kama za kufunga karanga wao wanaruhusiwa kwa kutumia viwango vilivyotolewa TBS.

Kuhusu wajasiriamali wanaotumia vifungashio hivyo kufunga biashara za karanga, Jafo amewatoa hofu kwa kuwataka kuendelea na kutengeneza uchumi wao kwa kufuata utaratibu ambao umetolewa na TBS.

Amewataka watu kufuata sheria kwa sababu kukiuka sheria ni jambo baya na linaweza kuwaingiza hatiani.