Jela miaka 20 kwa kumbaka mwanaye

Mkazi wa Mbagala,Afidhi Mbunda akiwa ameshikiliwa baada ya kuhukumiwa kifungo cha miaka 20 jela kwa kumbaka mtoto wake mwenye umri wa miaka 18. Picha na Pamela Chilongola

Muktasari:

  • Mkazi wa Mbagala, Hafidhi Mbunda (43)  amehukumiwa kifungo cha miaka 20 jela na mahakama ya Wilaya ya Temeke baada ya kukutwa na hatia ya kumbaka mtoto wake mwenye umri wa miaka 18.

Dar es Salaam. Mkazi wa Mbagala, Hafidhi Mbunda (43)  amehukumiwa kifungo cha miaka 20 jela na mahakama ya Wilaya ya Temeke baada ya kukutwa na hatia ya kumbaka mtoto wake mwenye umri wa miaka 18.

Hukumu hiyo imetolewa leo Jumanne Aprili 13,2021 na hakimu mkazi, John Ngeka aliyebainisha kuwa Machi 3, 2021 mahakama hiyo ilipokuwa ikisoma hukumu ilimtia hatiani mshtakiwa huyo kwa kumbaka mtoto mwanaye.

Amebainisha kuwa baada ya kutiwa hatiani mshtakiwa alizimia na mahakama iliahirisha shauri hilo na kuamuru mshtakiwa apelekwe hospitali ya Jeshi la Magereza akiwa chini ya ulinzi.

Amesema baada ya kupitia ushahidi wa upande wa utetezi na mashtaka akiwemo muhanga mwenyewe mahakama hiyo haikuwa na shaka hivyo mshtakiwa huyo alimbaka binti  huyo.

Alibainisha kuwa mshtakiwa alikuwa amembaka binti yake mwenye umri wa miaka 18,  mahakama imemuona ana hatia kwa mujibu wa kifungu 158 (1) (b) cha kanuni ya adhabu sura ya 16 marejeo ya mwaka 2019.

"Sheria hiyo inasema ukimwingilia mtoto wako kuanzia umri wa miaka 18 na kuendelea adhabu yake ni kifungo cha miaka 20 jela lakini akiwa chini ya miaka 18 adhabu yake ni miaka 30 jela," amesema Ngeka.

Ngeka amesema mtuhumiwa alikuwa anamuingilia mwanaye baada ya kuachana na mkewe.