Kadco kukusanya Sh17 bilioni

Muktasari:

Kampuni ya uendeshaji na uendelezaji wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Kilimanjaro (Kadco) imekusudia kukusanya  zaidi ya Sh17.5 bilioni mwaka 2021/22 na kutumia Sh15.5 bilioni kwa ajili ya  matumizi ya kawaida pamoja na mishahara ya watumishi.

Hai. Kampuni ya uendeshaji na uendelezaji wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Kilimanjaro (Kadco) imekusudia kukusanya  zaidi ya Sh17.5 bilioni mwaka 2021/22 na kutumia Sh15.5 bilioni kwa ajili ya  matumizi ya kawaida pamoja na mishahara ya watumishi.

Akizungumza leo Alhamisi Machi 4, 2021 katika ufunguzi wa baraza la wafanyakazi kaimu mkurugenzi wa kampuni hiyo, Christine Mwakatobe amesema kuanzia Julai 2020 hadi Januari 2021,  Kadco imekusanya zaidi ya Sh5 bilioni zilizotokana na tozo  za maegesho ya ndege na kodi mbalimbali.

Amesema katika kipindi hicho hawakutegemea mfuko wa Serikali kujiendesha.

Amebainisha kuwa  mwaka wa fedha 2021/22 wamekadiria kukusanya zaidi ya Sh17.5 bilioni na matumizi  na mishahara ya watumishi, watatumia zaidi ya Sh15.5 bilioni.

Amesema katika fedha hizo Kadco imekusudia kuboresha baadhi ya miradi ya maendeleo itakayogharimu Sh1.95 bilioni.

"Ipo miradi ambayo tumenuia kuikamilisha ndani ya miaka mitano ikiwamo kujenga hoteli ya nyota tano pamoja na business complex na kuanzisha mradi wa ufugaji wa nyuki,” amesema.

Akifungua baraza la wafanyakazi wa Kadco mkurugenzi wa utawala  na rasilimali  watu wizara  ya ujenzi na uchukuzi, Lucas kambelenje amesema aliwataka watumishi wasimamia vizuri mapato na matumizi waweze kutoka kwenye kampuni na kuwa taasisi ya umma.