Kahama yazipiku wilaya 149 mbio za Mwenge 2021

Miradi ya Sh15.3 bilioni yakataliwa na Mwenge wa Uhuru

Muktasari:

  • Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga imeibuka kidedea kwa vigezo vya ubora wa usimamizi na utekelezaji wa miradi ya maendeleo wakati wa mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu.

Chato. Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga imeibuka kidedea kwa vigezo vya ubora wa usimamizi na utekelezaji wa miradi ya maendeleo wakati wa mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu.

Umwamba wa Kahama dhidi ya wilaya zingine 149 zilizotembelewa na mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu umetangazwa leo Alhamisi Oktoba 14, 2021 na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na wenye Ulemavu), Jenista Mhagama wakati wa maadhimisho ya kilele cha mbio hizo zinazofanyika mjini Chato.

Waziri Mhagama amezitaja Wilaya zingine zilizoibuka na ushinda wa kikanda kuwa ni Nyamagana, Shinyanga, Muleba, Ruangwa na Kusini Unguja.

Wilaya hizo pamoja na mikoa ya Kusini Unguja na Geita zilizokuwa wenyeji wa sherehe za uzinduzi na hitimisho wa mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu zimepata zaidi ya vyeti, vikombe na fedha taslimu.