Kamati yaundwa kuchunguza chanjo moto sekondari ya Bumangi

Kamati yaundwa kuchunguza chanjo moto sekondari ya Bumangi

Muktasari:

Mkuu wa mkoa wa Mara,  Adam Malima ameunda kamati kwa ajili ya kuchunguza moto ulioteketeza bweni la wavulana la shule ya Sekondari Bumangi iliyopo wilayani Butiama.

Butiama. Mkuu wa mkoa wa Mara,  Adam Malima ameunda kamati kwa ajili ya kuchunguza moto ulioteketeza bweni la wavulana la shule ya Sekondari Bumangi iliyopo wilayani Butiama.

Malima amesema lengo la kuundwa kwa kamati hiyo ni kubaini chanzo cha moto huo ulioteketeza bweni lililokuwa likitumiwa na wanafunzi 127 wa kidato cha tano na sita katika shule hiyo.

Akizungumza baada ya kutembelea eneo la tukio,  Malima amesema moto huo umezua maswali mengi kwa kuwa bweni hilo na ukweli kuwa bweni hilo  lilifungwa saa 12.50 jioni ili wanafunzi waende darasani kwaajili ya vipindi vya dini.

Amesema dakika kumi baada ya bweni hilo kufungwa moto uliibuka na kuenea kwenye jengo lote ilhali  hakukuwepo  na mwanafunzi yeyote bwenini na kubainisha kuwa huduma za umeme katika bweni hilo zilikuwa zimeondolewa zaidi ya wiki mbili kutokana na matatizo yanayodaiwa kuwa ni ya kiufundi.

Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Mara,  Augustino Magere amesema  wameanza kufanya uchunguzi juu ya tukio hilo lilitokea Novemba 23 saa 1 usiku na kuteketeza kila kitu ndani ya bweni hilo .

Amesema hadi sasa chanzo cha moto huo hakijafahamika, “katika tukio hilo mwanafunzi mmoja alipoteza fahamu kutokana na taharuki na kupelekwa katika zahanati ya kijiji cha Bumangi ila hali yake iliimarika na kurudishwa shuleni jana hiyo.”

Wakizungumza shuleni hapo baadhi ya wanafunzi wameiomba serikali kuwapa msaada wa haraka kwani wamepoteza kila kitu.