Kamati za Bunge zatumia SGR mpya Dodoma-Dar

Mkurugenzi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Masanja Kadogosa akitoa maelekezo ndani ya treni iliyobeba wabunge wanaokagua Miundombinu ya Ujenzi wa SGR.

Muktasari:

Kamati ya Bunge ya Miundombinu wameanza safari ya kutoka Dodoma kuelekea Morogoro kwa njia ya treni wakipita Reli mpya ya SGR.

Dodoma. Kamati za Bunge za Miundombinu na Hesabu za Serikali (PAC) wameanza safari ya kutoka Dodoma kwenda Morogoro kwa njia ya treni wakipita reli mpya ya kisasa (SGR).

 Wabunge hao wanapitia reli hiyo kwa ajili ya ukaguzi wa hatua ya ujenzi wa reli ya mwendo kasi ilipofikia ambapo safari imeongozwa na Mkurugenzi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Masanja Kadogosa, leo Jumatatu, Septemba 26, 2022.

Hii itakuwa mara ya kwanza kwa reli mpya kupitia na treni kwa mwendo mrefu kutoka Dodoma - Morogoro hadi Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa kuanza safari hiyo, Kadogosa amewaambia wabunge ujenzi wa reli hiyo kutoka Dodoma hadi Dar es Salaam upo katika hatua nzuri na ifikapo Desemba 2022 treni ya mwendo kasi inaweza kusafiri kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma.

Hata hivyo, wabunge wametumia treni ya kawaida kwenye reli hiyo mpya hivyo mwendo wake ulikuwa wa kawaida si kasi kama ambavyo itapita juu tren mpya.

Wabunge wanapewa taarifa ya hatua za ujenzi kwa kila kituo hasa kwenye vituo vya kupozea umeme.