Kauli ya Tanroads ujenzi barabara Nachingwea-Masasi

Kauli ya Tanroads ujenzi barabara Nachingwea-Masasi

Muktasari:

  • Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) Mkoa wa Lindi umesema hakuna siasa wala uongo katika ujenzi wa barabara ya Nachingwea kwenda Masasi  kwa kiwango cha lami.

Lindi. Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) Mkoa wa Lindi umesema hakuna siasa wala uongo katika ujenzi wa barabara ya Nachingwea kwenda Masasi  kwa kiwango cha lami.

Hayo  yameelezwa  leo  Jumamosi Septemba 11, 2021 na meneja wa wakala huyo mkoani humo,  Ephatar Mlavi katika kikao chake na wanahabari.

Mlavi  amesema Serikali imedhamiria kujenga barabara hiyo na imeipa umuhimu mkubwa.

"Kwa hiyo hakuna uongo wala siasa katika ujenzi wa barabara hii inayounganisha  wilaya ya Nachingwea mkoani Lindi na  masasi mkoani Mtwara, " amesema.

Amebainisha kuwa upembuzi yakinifu umekamilika  kinachosubiriwa ni fedha ili ujenzi uanze na kwamba ujenzi wa barabara ya Nanganga-Ruangwa unaendelea baada ya kuwa na timu mbili  moja ikijenga  kutoka Nandagala kwenda Ruangwa na timu mbili zinaelekea Nanganga.


Amesema  kazi ngumu si kuweka lami bali kuchonga milima na kujaza udongo kwenye mabonde.


"Ujenzi umeanzia  katika kijiji cha Nandagala kutokana na  mkandarasi kuweka kambi katika kijiji hicho ambacho kipo katikati ya Ruangwa na Nanganga, " ameeleza akigusia matengenezo katika maeneo korofi  barabara za Ngongo-Ruangwa, Tingi-Kipatimo eneo la mlima Ngoge na Nangurukuru-Liwale.