Lushoto yatengewa Sh3.4 bilioni za maendeleo, mapambano ya Uviko-19

Mkuu wa Wilaya ya Lushoto Mkoani Tanga, Kalisti Lazaro.

Muktasari:

  • Mkuu wa Wilaya ya Lushoto Mkoani Tanga, Kalisti Lazaro amesema Wilaya hiyo imetengewa kiasi cha fedha Sh3.4 bilioni za Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya Uviko-19.

Lushoto. Mkuu wa Wilaya ya Lushoto Mkoani Tanga, Kalisti Lazaro amesema Wilaya hiyo imetengewa kiasi cha fedha Sh3.4 bilioni za Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya Uviko-19.

Akizungumza leo Oktoba 14 katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Kisiwani na Kata ya Mayo katika Halmashauri ya Bumbuli, Kalisti amesema fedha hizo ni sehemu ya Sh1.3 trilion zilizotolewa na serikali hivi karibuni.

Mkuu huyo wa Wilaya alisema fedha hizo zitaelekezwa katika utatuzi wa changamoto mbalimbali ikiwemo ya upungufu wa madarasa, nyumba za Walimu na hivyo kufanya wanafunzi watakaojiunga na kidato cha Kwanza kuondokana na changamoto hiyo.

"Tunaishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa kutupatia wana Lushoto fedha hizo.  kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za watumishi, ununuzi wa mashine za mionzi (X-Ray), elimu msingi, elimu maalum, vyumba vya madarasa katika vituo shikizi, madarasa ya sekondari na miradi ya maji," alisema Kalisti.

Akitoa mchanganuo wa fedha hizo, DC Kalisti amesema kwenye ujenzi wa nyumba za watumishi Halmashauri ya Bumbuli na Lushoto kila moja imepatiwa Sh90 milioni.