Maadhimisho ya Wiki ya Unyonyeshaji Duniani 2022
Muktasari:
Wiki ya Unyonyeshaji Duniani ni maadhimisho ya kila mwaka ambayo hufanyika kila mwaka kuanzia tarehe 1 hadi 7 Agosti katika nchi zaidi ya 120 ikiwemo Tanzania.
*Na Tuzie Edwin Ndekia
Wiki ya Unyonyeshaji Duniani ni maadhimisho ya kila mwaka ambayo hufanyika kila mwaka kuanzia tarehe 1 hadi 7 Agosti katika nchi zaidi ya 120 ikiwemo Tanzania.
Ni fursa ya kupigia chapuo na ushirikiano na wadau mbalimbali katika kukuza, kulinda na kusaidia unyonyeshaji.
Kauli mbiu ya Wiki ya Unyonyeshaji Duniani ya mwaka huu, “Ongeza Unyonyeshaji: Elimisha na Saidia,” inatukumbusha umuhimu wa kusimamia unyonyeshaji na kuhakikisha kuwa wanawake wanapata taarifa na msaada muhimu
.Maziwa ya mama ni bora
Maziwa ya mama hutoa virutubisho vyote ambavyo mtoto mchanga anahitaji katika miezi sita ya kwanza ya maisha; huwa kama chanjo ya kwanza kwa watoto wachanga, kuwalinda kutokana na magonjwa na maambukizi mbalimbali.
WHO na UNICEF zinapendekeza kwamba watoto waanze kunyonyeshwa ndani ya saa ya kwanza baada ya kuzaliwa, kunyonyesha maziwa ya mama pekee kwa muda wa miezi sita ya maisha (maana yake hakuna vyakula au vinywaji vingine vinavyotolewa, ikiwa ni pamoja na maji), ikifuatiwa na kuendelea kunyonyesha hadi miaka miwili au zaidi.
Kuanzishwa kwa unyonyeshaji kwa wakati ndani ya saa moja baada ya kuzaliwa kunaweza kuzuia asilimia 22 ya vifo vya watoto wachanga, na kutoa ulinzi mkali dhidi ya aina zote za utapiamlo wa watoto, ikiwa ni pamoja na kupoteza na kunenepa kupita kiasi.
Watoto ambao hawanyonyeshwi katika miaka ya kwanza ya maisha wana uwezekano mkubwa wa kupata magonjwa ya kawaida kama vile kuhara, nimonia na pumu, ambayo husababisha idadi kubwa ya vifo vya watoto kila mwaka.
Unyonyeshaji pia hutoa faida za kiafya kwa wanawake kwa sababu husaidia kutenganisha uzazi, hupunguza hatari ya saratani ya matiti na shingo ya kizazi na shinikizo la damu, husaidia katika kupona baada ya kuzaa na kupunguza uzito, na kunahusishwa na unyogovu mdogo baada ya kuzaa.
Kuvunja vikwazo
Imani ya kwamba kunyonyesha mtoto maziwa ya mama pekee haitoshi, mila zinazohitaji watoto wachanga kupewa vyakula maalum baada ya kujifungua (ili kuwakaribisha duniani), uuzaji wa bidhaa za lishe kwa watoto wachanga, ukosefu wa msaada wa kutosha kwa mzigo mkubwa wa kazi, pamoja na utoaji wa likizo ya uzazi usiotosheleza ni vikwazo kwa akina mama.
Ni muhimu kwa akina mama kuhisi kuungwa mkono na kutiwa moyo na mazingira yao ya karibu, ambayo yanajumuisha wenzi wao, familia, wahudumu wa afya, jamii, waajiri wao na vyombo vya habari, kwa manufaa ya mama na mtoto.
*Ofisa Lishe, UNICEF Tanzania